Patanisho: Dada wa mamangu alinilea lakini nikaanza kulewa na kumkosea heshima

"Yeye ndiye alinisomesha from class 6 hadi class 8 then nilipomaliza shule nikaanza kulewa huko kwake maeneo ya Bomet. Naona nilimkosea sana na ningependa nimuombe msamaha,” Koech alisema

Muhtasari

• Alisema kwamba kilichomkasirisha Zaidi mamake mdogo ni kumuingiza mtoto wa shangazi yake katika ulevi.

GHOST NA GIDI STUDIONI
GHOST NA GIDI STUDIONI GHOST NA GIDI STUDIONI
Image: RADIO JAMBO

Ijumaa ya Septemba 22, katika kipindi cha Gidi na Ghost asubuhi kitengo cha Patanisho, jamaa kwa jina Hillary Koech kutoka Nakuru mwenye umri wa miaka 28 aliomba kupatanishwa na mamake mdogo kwa jina Joyce Ng’eno mwenye umri wa miaka 40 kutoka Bomet baada ya kile alisema alimkosea heshima.

Koech alisema kwamba mamake mdogo huyo alimsomesha kutoka darasa la 6-8 lakini baada ya kumaliza shule, alianza kulewa na kumkosea heshima mama mdogo nyumbani kwake Bomet.

“Nilimkosea sana Mama mdogo on Nov 2022 baada ya yeye ndiye alinisomesha from class 6 hadi class 8 then nilipomaliza shule nikaanza kulewa huko kwake maeneo ya Bomet. Naona nilimkosea sana na ningependa nimuombe msamaha,” Koech alisema.

“Huyu ni dada ya mamangu alinifadhili wakati nilimaliza darasa la 8 nikatoka huko na sikuenda sekondari. Nikaanza mambo ya kulewa. Baadae akaniita huko kwake akaniambia nilikuwa kijana mzuri niende nimsaidie. Kufika huko nikaanza kulewa tena. Alikuwa ananipa pesa,” Koech alisema.

Alisema kwamba kilichomkasirisha Zaidi mamake mdogo ni kumuingiza mtoto wa shangazi yake katika ulevi.

Baadae alitoka kule na akamuacha mtoto wa shangazi kama ni mlevi chakari na kutoka kwake hakuwaambia jambo ambalo lilimfanya kuhisi kwamba alikosea sana.

“Nilikuwa nakunywa hii pombe kali kali, hata chang’aa lakini niliacha mwaka huu Machi. Mimi sitaki kumuomba mama mdogo msamaha kwa sababu nataka kurudi, hapa Nakuru niko na kazi yangu,” Koech ambaye hajaoa alisema.

Joyce Ng’eno alipopigiwa simu, alikubali kuzungumza na Hillary Koech na akamuuliza Koech kama ameamua kurekebika na kuacha pombe kabla ya kumsamehe.

“Ubadilike kabisa, uende kanisa ufanye kazi yako ili usaidie familia yako. Mimi sina shida na wewe nimekusamehe, hata sikuwa nimekuchukia ni wewe tu ulienda ukanyamaza sababu ulijua makosa yako,” Mama Joyce alimwambia Koech.