Patanisho: "Akiacha, mambo yataenda sawa!" Baba ashikilia baraka za mwanawe kwa sababu ya ulevi

Evans alidai amejaribu sana kuacha ulevi lakini kila anapopata pesa anajipata kwenye majiribio ya kukunywa tena.

Muhtasari

•Evans alisema uhusiano wake na Mzee Juma uliharibika kufuatia tabia yake ya ulevi ambayo mzazi huyo wake hapendi kabisa.

•Mzee Juma alikubali kumsamahe mwanawe ila akamshauri achukue muda kutafakari kuhusu maisha yake.

GHOST NA GIDI STUDIONI
GHOST NA GIDI STUDIONI GHOST NA GIDI STUDIONI
Image: RADIO JAMBO

Katika kitengo cha Patanisho, Evans Juma (27) alituma ujumbe akiomba kupatanishwa na baba yake mzazi, Bw James Juma (60) ambaye alikosana naye miezi mitatu iliyopita.

Evans alisema uhusiano wake na Mzee Juma uliharibika kufuatia tabia yake ya ulevi ambayo mzazi huyo wake hapendi kabisa na amekuwa akijaribu kumwagiza aache.

"Baba yangu tulikosana kisa ulevi. Nilikuwa nakunywa pombe nalewa. Yeye ni mtu wa kanisa, hapendi pombe. Alijaribu kunikataza lakini nikijaribu nashindwa kuwacha. Nimejaribu kadri ya uwezo wangu lakini nimewacha. Kabla ya kuwachana nayo, kuna pesa nikakula ikaisha. Ilikuwa wrong number nikakula ikaisha alafu nikashikwa. Ilikuwa elfu moja. Niliposhikwa alikuja akalipa pesa nikatoka," Evans alisema.

Evans alidai kwamba amejaribu sana kuacha ulevi lakini kila anapopata pesa anajipata kwenye majiribio ya kukunywa tena.

"Niliwacha pombe mwezi uliopita. Ni vile sina pesa saa hii. Sina pesa saa hii, nikipata naona kama naweza kunywa tena. Baba yangu mzazi hataki pombe kabisa. Naweza pata lakini nikipata naona kama nitakunywa. Nakunywa pombe kimpango, haijaathiri kazi yangu. Nilimwambia tunafaa tukae chini tujadiliane kuhusu hili na tusulihishe. Nilimwambia kupitia kwa redio nataka tujadiliane tuongee," alisema.

Mzee Juma alipopigiwa simu, Evans alitumia fursa hiyo kumwomba msamaha kufuatia tabia yake ya ulevi.

"Nilikuwa nakuomba msamaha baba yangu kuhusiana na pombe na pesa ambazo ulinikopesha. Naomba msamaha," Evans alimwambia baba yake.

Mzee Juma alimwambia, "Na sio eti ulikosea, mbona ata hukutuma mtu akuje nimskie tuongee. Lakini ni sawa kama unataka tuongee. Mambo najaribu kukukataza unaendelea. Lakini nakupenda, napenda familia yangu. Shida yako, kila nikiongea unaenda kinyume. Usingeongea, Mambo yako yasingeenda vizuri."

Aliongeza, "Mimi nilinyamaza kwa sababu nimejaribu kuongea na yeye haskii. Nilimwambia akiendelea, mambo yake hayataenda sawa. Aliposhikwa nilitumia lugha mpaka akatoka.. Anastahili kujipanga. Maamuzi ni yake. Yeye ndiye anafaa kujiamulia mwenyewe. Aachane na pombe, hiyo ndo vita kati yangu na yeye. Akiacha pombe mambo yake yataenda sawa. Kuna asilimia nimefunga lakini akiwacha nitafungua, yeye hajui."

Mzee Juma hata hivyo alikubali kumsamahe mwanawe ila akamshauri achukue muda kutafakari kuhusu maisha yake.

"Nimemsamehe, sina shida na yeye. Ajihoji, ajue hili ni nzuri ama mbaya," Mzee Juma alisema.

Evans alisema, "Nimewacha pombe. Ata mwisho wa mwezi nikipata pesa sitakunywa."