Patanisho: Jamaa amfukuza mkewe baada ya kumdanganya yuko nyumbani ilhali mama mkwe asharipoti hayupo

"Sijui kama ananishuku kuwa na mpango wa kando, lakini yeye mwenyewe hajaniambia," Nancy alisema.

Muhtasari

•Nancy alisema ndoa yake ya mwaka mmoja ilivurugika alipomdanganya mumewe kuwa yuko nyumbani ilhali alikuwa njiani.

•Nancy alisema anajuta sana kumdanganya mume wake na kuomba asaidiwe kuomba msamaha ili kurejesha mahusiano yao

Image: RADIO JAMBO

Mwanadada aliyejitambulisha kama Nancy Kaunda ,21, kutoka Migori alituma ujumbe akiomba kupatanishwa na mume wake Boniface Onyango ,27, ambaye alikosana naye mapema wiki hii baada ya kumdanganya.

Nancy alisema ndoa yake ya mwaka mmoja ilivurugika alipomdanganya mumewe kuwa yuko nyumbani ilhali alikuwa njiani.

"Nilikuwa nimeenda clinic siku ya Jumatatu.Nikapitia kwa rafiki yangu na nikatoka nimechelewa. Mume wangu alipiga simu akiuliza niko wapi, nikamwambia nimefika kwa nyumba lakini bado nilikuwa njiani. Kumbe alikuwa ashaongea na mama yake akamwambia sijafika. Alisema nichukue vitu zangu niende nyumbani. Lakini mama mkwe alikataa niende," Nancy alisema.

Nancy alisema anajuta sana kumdanganya mume wake na kuomba asaidiwe kuomba msamaha ili kurejesha mahusiano yao.

"Anafanya kazi Nairobi. Nilimuona mara ya mwisho mwezi wa nane. Sijui kama ananishuku kuwa na mpango wa kando, lakini yeye mwenyewe hajaniambia. Sasa hivi haniongeleshi vizuri, wakati mwingine nikimpigia simu hachukui," alisema.

Juhudi za kuokoa ndoa ya Nancy hata hivyo hazikufaulu kwani simu ya Boniface haikuingia alipopigiwa na Gidi.

"Tungekuwa tunaongea ingekuwa ni sawa. Nitajaribu kuongea na mama mkwe," Nancy alisema.

Alipopewa fursa ya kuzungumza na mumewe hewani, alisema, "Namuomba msamaha najua nimemkosea. Turudiane, tuishi pamoja. Mimi bado nampenda."

MJADALA;

Je, ni vyema kwa wanandoa walio kwenye mahusiano ya mbali kufuatiliana?