Patanisho: Jamaa akiri kufukuzwa Uarabuni kutokana na utundu baada ya kutafutiwa kazi na shangaziye

"Ilikuwa nifanye kazi alafu baada ya miaka miwili nimrudishie hela zake.Nilifanya kazi kiasi alafu nikafutwa nikarejeshwa Kenya," Eric alisema.

Muhtasari

•Eric alisema shangazi yake alikuwa amejitolea kumtafutia  kazi nchini Qatar lakini utundu wake ukafanya akafutwa baada ya kipindi kifupi.

•"Nilikuwa naskia niko na makosa sana. Najua ungesaidia wengine. Asante kwa kunisamehe, sitakuangusha tena," Eric alimwambia shangazi yake.

Ghost na Gidi
Ghost na Gidi
Image: RADIO JAMBO

Kijana aliyejitambulisha kama Eric Njuguna ,25, kutoka Dagoretti Market alituma ujumbe akiomba kupatanishwa na shangazi yake Eunice Karwenji ambaye alikosea sana takriban mwaka mmoja uliopita.

Eric alisema shangazi yake ambaye ni ajenti wa kazi za Uarabuni alikuwa amejitolea kumtafutia  kazi ya ulinzi nchini Qatar wakati wa Kombe la Dunia lakini utundu wake ukafanya akafutwa kazi baada ya kipindi kifupi.

"Shangazi yangu alinipeleka Qatar kufanya kazi na akanilipia ada zote. Ilikuwa nifanye kazi alafu baada ya miaka miwili nimrudishie hela zake.

Nilifanya kazi kiasi alafu nikafutwa nikarejeshwa Kenya. Nilikuwa nimeenda November 18 wakati wa World Cup ," Eric alisimulia.

Aliongeza, "Hao Waarabu walisingizia nilikuwa mkali sana na nilitaka kupigana na mwenzangu. Lakini kwa kweli hatukupigana. Nilikuwa Doha, Qatar kazi ya ulinzi. Nilikuwa nataka kumuomba shangazi yangu msamaha kwa sababu tangu nirudi Kenya hatujazungumza na kujadiliana jinsi nitarejesha hela zake."

Eric alisema walikuwa wamekubaliana na shangazi yake kwamba wangekutana jijini Nairobi ili kusuluhisha mzozo wao ila mkutano huo haukuafikiwa.

Bi Eunice alipopigiwa simu, Eric alichukua fursa hiyo kumuomba msamaha, "Auntie nakuomba msamaha kwa kuharibu pesa na wakati wako na. Kwa kweli sio mapenzi yangu na makosa waliniwekea sio ya kweli. Nilijaribu sana kueleza yaliyotokea lakini hawakuniskia. Jamaa ambaye walidai tumepigana naye alikuwa wa kampuni nyingine na walikuwa wakimtetea. Naomba unisamehe tafadhali."

Bi Eunice ambaye alisikika mpole na mtulivu alikubali ombi la msamaha la mpwa huyo wake na kumwambia, "Nimekusamehe, na hata nilikusamehe kitambo kwa sababu kwa kweli hakukuwa na thibisho kwamba ulifanya hayo makosa. Najua vile umelelewa na najua huwezi kufanya makosa hayo. Nilikusamehe na ujiskie ukiwa huru. Tutajaribu tena mpaka usimame tena. Ujiskie kwamba umesamehewa."

Eric, kwa furaha tele alimshukuru shangazi yake na kumwambia, "Nilikuwa naskia niko na makosa sana. Najua ungesaidia wengine. Asante kwa kunisamehe, sitakuangusha tena."

Je, una maoni yepi kuhusu Patanisho ya leo?