"Hajui mtoto anakula nini, anavaa nini!" Mama mkwe amlalamikia jamaa aliyetoroka na bintiye

Mama mkwe alimtaka Etyang ashughulikie mtoto wake huku akifichua kwamba aliwahi kutuma Sh500 pekee.

Muhtasari

•Etyang alisema uhusiano wake na mama mkwe uliharibika mwaka wa 2022 wakati alipomtunga mimba binti yake.

•Bi Mary Manyonge alipopigiwa simu aliweka wazi kwamba tayari alimsamehe na hana uhasama wowote dhidi yake.

Image: RADIO JAMBO

Luka Etyang kutoka kaunti ya Busia alituma ujumbe akiomba kupatanishwa na mke wake Mary Mayonge ,48, ambaye alikosana naye takriban miaka miwili iliyopita.

Etyang alisema uhusiano wake na mama mkwe uliharibika mwaka wa 2022 wakati alipomtunga mimba binti yake kisha baadaye kumtumia ujumbe mbaya kwa simu. 

"Mwaka wa 2022,  kuna msichana nilipachika mimba wa area ya nyumbani. Tulikaa naye mpaka akajifungua. Baadaye niliondoka na msichana nyumbani tukaenda Nairobi ili kutafuta kazi. Mtoto tuliacha na mama mkwe,"  Etyang alisimulia.

Aliendelea, "Mama alikuwa anapiga simu akitaka bintiye arudi nyumbani. Niliambia mama mkwe sitaki kusumbuliwa kwa simu kila siku. Kuanzia huo mwezi wa saba mwaka jana tumekuwa tukiongea lakini sio sana. Uhusiano uliharibika." 

Etyang alisema ni baada ya kupokea ujumbe kutoka kwa wakwe zake wakitaka msichana wao arudi nyumbani ambapo alimwandikia mama mkwe ujumbe mbaya.

"Nilijibu meseji nikasema msichana hawezi kurudi. Kwa saa hii siishi na yeye juu alipata kazi ambayo anafanya. Huwa tunapatana wikendi. Huwa namshughulikia mtoto lakini sio mara nyingi sana. Sijamuoa rasmi," alisema.

Alisema angependa kupatana na mama mkwe kwa sababu hawezi kuishi na msichana ilhali haelewani na mama yake.

Bi Mary Manyonge alipopigiwa simu aliweka wazi kwamba tayari alimsamehe na hana uhasama wowote dhidi yake.

"Ata mimi nilikusamehea kitambo, sina makosa na wewe. Wewe unaogopa kupiga simu usalimie mtoto wako," Bi Mary alisema.

Etyang alisema alichukua hatua ya kuomba msamaha kwa kuwa alihisi alikosea kwa kutuma ujumbe wa matusi.

Bi Mary alimwambia, "Mara nyingine nipigie simu tunaongea na tunasaidiana. Wewe ni kama mtoto wangu ambaye nimebeba kwa tumbo yangu. Ata mimi nimekusamehea kabisa"

Aliongeza, "Niko na mtoto wake, ndiyo maana nampatia heshima. Ata kama alikosea mtoto wangu siwezi nikamuonyesha madharau. Mtoto sasa ako ni miaka miwili."

Mama mkwe hata hivyo alimtaka Etyang ashughulikie mtoto wake huku akifichua kwamba aliwahi kutuma Sh500 pekee.

"Hajui mtoto wake anavaa aje, anakula aje, mpaka akuwe mkubwa. Mimi siwezi kukatalia mtoto wake," Bi Mary alisema.

Etyang alisema, "Nawatambua kama wakwe zangu na nawapenda sana. Nilikuwa tu nataka kuomba msamaha."

Kwa upande wake, Bi Mary alisema, "Wewe mwenyewe ndiye ulikuwa unaogopa. Hata kwa Mungu nilishakusamehe."