"Hiyo ni Kamúti!" Gidi astaajabu mwanadada kutaka kumrudia mpenziwe licha ya madharau chungu nzima

"Pesa yake huwa sishiki. Huyo hata nikimwambia nunua panty uniletee, anasema hizo vitu hawezi kununua," Janet alisema.

Muhtasari

•Janet alisema aligura ndoa yake ya miaka miwili mwezi Februari mwaka huu kutokana na madai ya madharau ya mumewe.

•"Huyo ni mtu mkikosana na yeye jioni analeta mwingine. Ata alikuwa analeta wanawake nikiwa. Ananiambia nilale kwa kiti na mtoto, wao wanalala kwa kitanda," alisema Janet.

GHOST NA GIDI STUDIONI
GHOST NA GIDI STUDIONI GHOST NA GIDI STUDIONI
Image: RADIO JAMBO

Mwanadada aliyejitambulisha kama Janet Mukunu ,21, kutoka kaunti ya Makueni alituma ujumbe akiomba kupatanishwa na mume wake Simon Mutua ,23, ambaye alikosana naye mapema mwaka huu.

Janet alisema aligura ndoa yake ya miaka miwili mwezi Februari mwaka huu kutokana na madai ya madharau ya mumewe.

"Mume wangu ni mtu ako na pikipiki. Lakini ukiugua anakwambia uende hospali kwa miguu. Siku moja niliugua nikampigia simu nikamwambia nimelewa, aliniambia nitembee kwa miguu.  Nilizidiwa nikapata kizunguzungu nikazimia. Watu wa kwetu wakapigiwa simu wakanikujia. Baadaye mume wangu alienda akatoa nguo zangu kwake akapeleka kwetu. Kwetu hakuna wazazi. Nashindwa nitafanya nini," Janet alisema.

Aliongeza, "Dadangu aliuza kuku akanitumia nauli nikaenda kwake. Huku nakwo ni shida. Mume wake ako Nairobi, pesa anayotuma ya chakula haitoshi.  Mtoto ni mgonjwa sana, nikimwambia mume wangu anasema nimpelekee mtoto atalea."

Alipoulizwa sababu ya kutaka kurudiana na mzazi huyo mwenzake licha ya madharau yote aliyopitishiwa, Janet alisema, "Namtaka juu niko na mtoto wake, lakini bado nampenda. Mwanaume mwenye alinitoa shule. Roho yangu inaniambia nirudi kwake."

Simon alipopigiwa simu aliweka wazi hataki mambo ya mzazi huyo mwenzake akimshtumu kwa kuwakosea heshima jamaa zake.

"Mtu mwenyewe anatusi watu. Ata anatusi wazazi nyumbani mpaka nakosana nao. Sijui shida yake ni nani. Huwa anaanza kutusi nyanya na shangazi hapo nyumbani," Simon alisema.

Kuhusu sababu ya kutompeleka mkewe hospitali kutumia pikipiki yake, alisema, "Yeye alikuwa na pesa inaweza kumpeleka kazi. Mimi nilikuwa nimeitiwa kazi kwingine."

Janet hata hivyo alipuuzilia mbali madai ya kuwatusi wanafamilia wa mumewe. Pia alipinga madai ya mumewe kuhusu sababu ya kutompeleka hospitali.

"Bibi wa kwanza ulisema alikuwa mbaya, pia mimi nimekuwa mbaya?. Nilikwambia unibebe unipeleke hospitali ukabeba wanaume wengine mkaenda. Nikawapata mkiwa mmekaa chini mahali. Hakuna kazi ulienda," alisema.

Simon hata hivyo alimwambia, "Mimi siwezi kurudiana na wewe" kisha akakata simu.

Janet aliendelea kulalamika, "Pesa yake huwa sishiki. Huyo hata nikimwambia nunua panty uniletee, anasema hizo vitu hawezi kununua. Nikimwitisha pesa nikanunua, hataki."

"Huyo ni mtu mkikosana na yeye jioni analeta mwingine. Ata alikuwa analeta wanawake nikiwa. Ananiambia nilale kwa kiti na mtoto, wao wanalala kwa kitanda," aliongeza.

Licha ya kuibua malalamishi mengi dhidi ya mpenziwe, Janet alisistiza kuwa bado anampenda na angependa warudiane.

Gidi alisema, "Hii ni kamuti. Huwezi kupenda mtu anakufanyia madharau kama hiyo. Hata baada ya kusema hakutaki, bado unasisitiza? Hiyo ni kamuti imechanganywa mpaka ikaongezwa ladha."

Gidi alimshauri aachane na jamaa huyo na akamtaka atumie sheria kumshinikiza ashughulikie mtoto.

Je, ushauri wako kwa Janet ni upi?