"Ilikuwa tuoane Disemba" Mwanadada akiri kumpenda sana jamaa ambaye hajawahi kukutana naye

"Disemba ilikuwa tuoane. Huwa nazungumza na mamake. Mamake aliniambia niende nyumbani," Vivian alisema.

Muhtasari

•Vivian alifichua maelezo ya kushangaza kwamba hajawahi kukutana na jamaa huyo, na ameona picha yake tu kwenye Facebook.

•"Hatujawahi kutana na yeye kabisa lakini nampenda hivyo. Alinitumia picha kwenye Facebook kitambo nikamuona, namjua. Sijawahi ona video yake. Lakini nampenda sana," Vivian alisema.

Gidi na Ghost Studioni
Image: RADIO JAMBO

Mwanadada ambaye alijitambulisha kama Vivian Nekesa ,22, kutoka kaunti ya Bungoma alituma ujumbe akiomba kupatanishwa na mchumba wake Dancan Kimutai ,27.

Vivian alisema uhusiano wake wa chini ya mwaka mmoja umetatizika kwani hawajakuwa wakielewana kwa muda.

"Hatuelewani. Nikimpigia simu, hatuelewani. Shida ni mawasiliano. Shida ingine ako nayo, anashinda kuchunga mtu kabisa. Wakati niko kazi nikimwambia nimetoka, anauliza nimeenda wapi. Ana wivu wa kimapenzi," Vivian alisema.

Vivian aliendelea kufichua maelezo ya kushangaza kwamba hajawahi kukutana na jamaa huyo, na ameona picha yake tu kwenye Facebook.

"Hatujawahi kutana na yeye. Tulijuana tu kwa simu. Nampenda. Hatujawahi kutana na yeye kabisa lakini nampenda hivyo. Alinitumia picha kwenye Facebook kitambo nikamuona, namjua. Sijawahi ona video yake. Lakini nampenda sana," Vivian alisema.

Aliongeza, "Disemba ilikuwa tuoane. Huwa nazungumza na mamake. Mamake aliniambia niende nyumbani. Nataka kumwambia nampenda. Juu wakati mwingine mi huwa na stress naona kama ananicheza.'

Duncan alipopigiwa simu, Vivian alimwambia, "Mi nakupenda, ni ile tu nataka nijue kama unanipenda. Nataka unihakikishie unanipenda, sijui unatakaje."

"Kila kitu iko sawa. Niko kazini Eldoret," Dancan alijibu.

Mtangazaji Gidi alimshauri Vivian aache mapenzi ya mitandaoni kwani anaweza kutapeliwa.

"Nilikuwa naplan kuenda chuo mwaka ujao. Nilikuwa tu nampenda," Vivian alisema.

Je, una maoni ama ushauri gani kuhusu Patanisho ya leo?