Patanisho: Jamaa akataa kumtumia mkewe nauli arudi baada ya kula Sh300 alizokuwa amemtumia

"Mimi si nilikwambia ukuje ukakata. Nikikutumia fare hukujangi. Nilikutumia fare ukasema unakuja hukuja," Baba Chebet alilalamika.

Muhtasari

•Mama Chebet  alisema ndoa yake ya mwaka mmoja ilivunjika mwaka wa 2021 baada ya mumewe kuanza kumshuku anaenda nje ya ndoa.

•Mama Chebet hata hivyo alipuuzilia madai ya mzazi huyo mwenzake kuwa amekuwa akimtumia nauli anakosa kurudi.

GHOST NA GIDI STUDIONI
GHOST NA GIDI STUDIONI GHOST NA GIDI STUDIONI
Image: RADIO JAMBO

Mwanadada aliyejitambulisha kama Janerose almaarufu Mama Chebet ,25, kutoka Bungoma alituma ujumbe akiomba kupatanishwa na mzazi mwenzake Baba Chebet ,32, ambaye alitengana naye takriban miaka miwili iliyopita.

Mama Chebet  alisema ndoa yake ya mwaka mmoja ilivunjika mwaka wa 2021 baada ya mumewe kuanza kumshuku anaenda nje ya ndoa.

"Nilikuwa nimeona na mwanaume huyo vizuri lakini ikafika mahali akaanza kunishuku. Marafiki wake wakikuja kutembea anaona kama wananikatia ilhali mimi sikuwa na haja na marafiki wake," Mama Chebet alisimulia.

Aliendelea, "Nilipata mimba na ilipofika kama miezi miwili nikatoka nikaenda nyumbani kwetu Bungoma. Sasa hivi mtoto amekuwa mkubwa lakini nikimpigia simu hatuelewani.. Hakusema mimba sio yake. Alikuwa anaona nimekaa tu na mtu ata marafiki zake anaanza kunishuku. Ata sikuwa nacheka na wao. Tulikuwa tunakaa kwa nyumba tu na tunapika chai. Mimi ndio namtafuta lakini nikimpigia simu ni maneno tu."

Mama Chebet alisema kwamba mzazi huyo wake amekuwa akimhakikishia kuwa bado hajapata mwanamke mwingine na amekuwa tu akimsubiri ila kila anapomuomba atume nauli hajakuwa akitimiza ombi lake.

Baba Chebet alipopigiwa simu aliweka wazi kuwa mkewe ndiye aliyetoroka nyumbani bila kufukuzwa.  Aidha, alidai amekuwa akimwambia Bi Janerose arejee nyumbani na hata kumtumia nauli ila hajawahi kurudi.

"Wewe ndiye ulipotea.Mimi si nilikwambia ukuje ukakata. Nikikutumia fare hukujangi. Nilikutumia fare ukasema unakuja hukuja," Baba Chebet alimwambia mkewe.

Mama Chebet hata hivyo alipuuzilia madai ya mzazi huyo mwenzake kuwa amekuwa akimtumia nauli anakosa kurudi.

Baba Chebet alifichua kwamba aliwahi kumtumia mkewe nauli ya shilingi mia tatu ila akakosa kurudi, jambo ambalo lilimfanya ahofie kuwa hi kumtumia tena.

"Yeye mwenyewe hatakangi kuja. Mimi mwenyewe nataka arudi... Niliona nikimtumia nauli tena atanidanganya atakuja. Nilimwambia atafute mahali atapata pesa akija nitamrudishia," Baba Chebet alisema.

Kwa kuwa mumewe alisema yuko tayari kumpokea tena nyumbani, Bi Janerose alisema angerejea baada ya kupata nauli.

"Mimi bado nakupenda. Siwezi nikalea mtoto nikiwa peke yangu," alimwambia Baba Chebet.

Baba Chebet alimwambia, "Nakupenda kama maharagwe."