Patanisho:"Siwezi kumsamehe!" Shangazi amtusi mpwa wake kwa kupachikwa mimba na shemeji yake

Rael alisikika kukasirishwa sana na mpwa huyo wake na kuweka wazi kuwa hataki kuzungumza naye.

Muhtasari

•Vallyne alisema uhusiano wake na shangazi yake ulidhoofika mwezi juni mwaka jana baada ya kupachikwa mimba na shemeji ya shangazi yake.

•Bi Rael alimuagiza mpwa huyo wake apige hatua ya kuenda nyumbani na kuzungumza na baba yake ili wapate kuelewana.

Image: RADIO JAMBO

Vallyne Chevukwa ,21, alituma ujumbe akiomba kupatanishwa na shangazi yake Rael Nafula ,45, ambaye alikosana naye mwaka jana kufuatia mzozo wa kinyumbani.

Vallyne alisema uhusiano wake na shangazi yake ulidhoofika mwezi juni mwaka jana baada ya kupachikwa mimba na shemeji ya shangazi yake ambaye ni mtoto wa bibi mdogo wa baba mkwe wa Bi Nafula.

"Nilikuwa naishi kwa shangazi mwaka jana Januari tukapatana na jamaa ambaye amezaliwa kwa nyumba ya pili ya baba mkwe wa shangazi kisha akanipa ujauzito mwezi wa nne. Nikatoka nikaenda kutafuta kazi. Shangazi alikuja kazini akanigombeza alafu akaenda. Mimi sina mama na yeye ndiye anaweza kunisaidia. Nilijifungua mwaka jana Novemba. Tunaishi na huyo jamaa. Shangazi yangu hakupenda," Vallyne alisema.

Aliongeza, "Sasa ikishafanyika, imefanyika. Mtoto alishapatikana. Kila mtu anajua."

Bi Rael alipopigiwa simu alisikika kukasirishwa sana na mpwa huyo wake na kuweka wazi kuwa hataki kuzungumza naye.

"Sitaki kuongea na yeye. Sitaki na sitaki na sitaki. Huyo mtoto ni mjinga sana. Siwezi kumsamehea hata kidogo. Mimi nimeoleka kwa boma. Mimi ndiye mkubwa. Kwa nyumba ndogo ameenda kwa kijana last born. Niliambiwa nimfukuze huyo msichana kwa boma. Tena walipigiana simu nikaskia ametoka kazinina akapata mimba. Siwezi kumsamehe," Bi Rael alisema.

Bi Rael alimuagiza mpwa huyo wake apige hatua ya kuenda nyumbani na kuzungumza na baba yake ili wapate kuelewana.

"Tena sitaki anipigie simu. Tumeolewa kwa boma moja. Huyo ni mtoto mjinga sana.Hasikiangi, alikataa kusoma akatoka nyumbani akaja hapa. Kukaa hapa, akaanza maneno aliyokuwa akifanya nyumbani. Siwezi kumsamehea hapa, sitaki hata kusikia sauti yake. Itakuaje ng'ombe wameletwa tena warudishwe kwao?," alilalamika Bi Rael kabla ya kukata simu na kutoweka hewani.

Vallyne ambaye alisikika kulemewa na hisai alisema, "Nilikuwa nataka kujua msimamo wake. Kama anakuwa mkali hivyo itakuwaje sasa."

Aliongeza, "Nakuomba msamaha. Nakutambua kama wewe ni mama yangu. Nimekuwa nikiishi na wewe. Tayari imetendeka. Naomba unisamehe haitawahi kutendeka tena."