In Summary

• Kabi alikiri alikuwa na wasiwasi mwingi alipokuwa anaenda kukutana na binti huyo wa miaka saba kwani alishindwa jinsi angejitambulisha kama babake.

•Mwanavlogu huyo alisema mke wake alimpatia nguvu ya kukabiliana na wasiwasi ambao alikuwa nao.

Image: INSTAGRAM// MILLY WA JESUS

Mwanavlogu na mfanyibiashara mashuhuri Peter Kabi almaarufu kama Kabi Wajesus amefunguka kuhusu mara ya kwanza walipokutana na binti yake Abby.

Akipokuwa kwenye mahojiano na Mungai Eve, Kabi alisema  mkutano  wake na bintiye ulikuwa wa kufana na alipata utulivu mkubwa moyoni.

Hata hivyo, Kabi alikiri alikuwa na wasiwasi mwingi alipokuwa anaenda kukutana na binti huyo wa miaka saba kwani alishindwa jinsi angejitambulisha kama babake.

"Nilikuwa na wasiwasi. Nilikuwa nashindwa ningesema nini. Tulikuwa na mpenzi wangu, nilikuwa namuuliza nitaambia Abby nini. Nilishindwa kama ningeenda nimwambie mimi ni baba yake. Nilishindwa ningevunja habari hizo vipi" Kabi alisema.

Mwanavlogu huyo alisema mke wake alimpatia nguvu ya kukabiliana na wasiwasi ambao alikuwa nao.

Hata hivyo alisema haikuwa ngumu sana kwani tayari mama ya binti yake, ambaye pia ni binamu yake alikuwa amemfahamisha anaenda kupatana  na baba yake.

"Nashukuru Mungu kwa kuwa angalau mama yake alikuwa  amemwambia anaenda kupatana na baba yake. Angalau haikuwa ngumu. Mama yake ameolewa, ana watotob wengine wawili" Kabi alisema.

Kabi alisema kabla ya kupatana na binti yake alishiriki kikao na mama Abby pamoja na mume wake ili kujadiliana kuhusu malezi yake.

Alisema  licha ya kuwa anafaa kuona binti yake kila baada ya wiki mbili, hilo halijawezekana sana kwa kuwa kumekuwa na vuta nikuvute kati yake na mama Abby.

"Nitaendelea kukazania hilo. Najua sio rahisi kwa hivyo sitarajii ukamilifu. Sitaraji kumuona kila wakati. Saa hii ni ngumu  kumuona lakini nikipata nafasi nitahakikisha tumekuwa na wakati mzuri pamoja"  Kabi alisema.

Aliweka wazi kwamba amekuwa akiwajibikia binti yake tangu wakati vipimo vya DNA vilibaini kuwa ndiye baba mzazi.

View Comments