In Summary

•Simple Boy ameweka wazi kuwa tayari ameweza kusonga mbele na maisha yake takriban miezi mitatu baada ya kutengana na Pritty Vishy.

•Amesema tayari kuna mpango wa wote wawili kuwatembelea wazazi wao kama sehemu ya mipango ya harusi.

Image: INSTAGRAM// STIVO SIMPLE BOY

Mwanamuziki mashuhuri Stivo Simple Boy ametangaza kwamba hatimaye amepata kipenzi cha maisha yake.

Simple Boy ameweka wazi kwamba tayari ameweza kusonga mbele na maisha yake takriban miezi mitatu baada ya kutengana na Pritty Vishy.

"Mimi siko single. Niko na mtu. Tayari nishamove on. Hivi karibu nitawaonyesha ni nani mwenye ameteka roho yangu," Stivo alisema katika mahojiano na Eve Mungai.

Rapa huyo kutoka Kibra alifichua kuwa yeye na mpenzi wake wa sasa wamefahamiana kwa muda mrefu na tayari wamefikia makubaliano ya ndoa.

"Saa hii nina mchumba mwenye ananipenda kwa dhati. Hivi karibuni tutarajie harusi. Pilau, Biryani na mapochopocho zote zitakuwa pale," Alisema.

Stivo alisema tayari kuna mpango wa wote wawili kuwatembelea wazazi wao kama sehemu ya mipango ya harusi.

Aidha alifichua kuwa alianza kuchumbiana na mchumba wake bado akiwa kwenye mahusiano na Vishy.

"Ni mnyenyekevu. Pia ni msichana ambaye anaelewa, anajua sitaki kitu anaelewa sitaki na kama napenda anajua napenda. Wiki ijayo tunaenda ajue familia yangu alafu pia mimi nijue familia yake," Alisema Stivo.

Msanii huyo alidai kwamba mwanadada anayechumbiana naye ana sifa zote ambazo alikuwa anatafuta kwa mke.

"Nimepata ambaye nilikuwa natarajia kwa maisha yangu. Mlango moja ikifunguka, ingine inafungulia. Nashukuru Mungu kwa kunipa mtu ambaye nilikuwa natarajia kwa maisha yangu," Alisema.

Mwezi uliopita Stivo akiwa kwenye mahojiano alidai kwamba bado anasubiri mtu bora zaidi wa kujitosa kwenye ndoa naye.

Alidokeza kuwa atakuwa tayari kushiriki tendo la ndoa kwa mara ya kwanza pindi tu atakapopata mwanamke sahihi wa kuoa.

"Kwanza lazima akuwa Mcha Mungu. Lazima akuwe mnyenyekevu, aniheshimu na pia mimi nimheshimu. Kama nimefanya kosa aniambie na pia akifanya kosa akubali," Alisema katika mahojiano na Oga Obinna.

Pia alifichua kuwa kuna wanadada wengi ambao wamekuwa wakimtongoza hasa kupitita mitandao ya kijamii.

Mapema mwaka huu mahusiano yake ya muda mrefu na Pritty Vishy yalifika hatima huku wote wawili wakinyoosheana kidole cha lawama.

View Comments