In Summary

•Seneta huyo ambaye tayari ana watoto wawili na Samidoh alibainisha kuwa bado hajafunga ukurasa wa kuzaa.

•Nyamu pia alieleza kufurahishwa na uwezo wa binti yake Wairimu wa kuongea akiwa na umri wa mwaka mmoja tu.

Image: INSTAGRAM// KAREN NYAMU

Seneta wa kuteuliwa Karen Nyamu amedokeza mpango wa kupata mtoto mwingine mmoja na mzazi mwenzake Samuel Muchoki almaarufu Samidoh.

Siku ya Jumatatu, wakili huyo ambaye tayari ana watoto wawili na mwimbaji huyo wa Mugithi aliweka wazi kwamba bado hajafunga ukurasa wa kuzaa.

Karen alifichua hayo baada ya mtumiaji wa Instagram kudokeza jinsi wanawe wawili wadogo wanavyofanana na baba yao.

"Yaani uliamua watoto wote wafanane na baba yao," shabiki alisema chini ya chapisho la Karen kwenye mtandao wa Instagram.

Bila kusita, seneta huyo alijibu, "Sijagive up. Najaribu one last time."

Kwenye chapisho lake la siku ya Jumatatu, Karen alionyesha binti yake na Samidoh, Wairimu akila aiskrimu na kusifia ujasiri wake.  Chini ya video hiyo, pia alimtaja mtoto wao wa kwanza Sam Junior kama mnyanyasaji.

"Haha Wairimu matihakagwo macuru (Wairimu huwa hawapakwi uji). Samy ni ka bully (Wairimu) amezoea kujilinda mwenyewe. Samy Samy mbaya," alisema.

Seneta huyo wa UDA pia alieleza kufurahishwa na uwezo wa Wairimu wa kuongea akiwa na umri wa mwaka mmoja tu.

"Nimefurahi kuwa akiwa na umri wa mwaka mmoja anaweza kuwasiliana .Hata kabla hajaweza kutembea. Ka genius haka," alisema.

Mzazi mwenzake Karen Nyamu, Samidoh ana watoto wawili na seneta huyo wa kuteuliwa na wawili na mke wake Edday Nderitu.

Wiki chache zilizopita, Nyamu alimsifia mwimbaji huyo kama baba mzuri na kuweka wazi kuwa anastahili watoto wengi. Alitoa kauli hiyo wakati akisherehekea siku ya kuzaliwa ya bintiye Edday Nderitu, Neriah Muchoki.

“Sawa kutokana na mahitaji ya umma hehehe. Baba mzuri anastahili watoto wengi. Heri ya kuzaliwa Neriah Muchoki,” alisema.

Seneta huyo wa kuteuliwa aliambatanisha ujumbe huo wa Facebook na picha zake, Samidoh na binti yao mdogo, Wairimu.

Nyamu na Samidoh walibarikiwa na mtoto wao wa kwanza pamoja, Sam Junior mwaka wa 2020 kabla ya kupata wa pili pamoja mwaka jana. Wawili hao wamedaiwa kuwa kwenye mahusiano ya siri kwa miaka kadhaa.

View Comments