In Summary

•Akothee alishangaa ni kwa nini watu wanajali sana mahusiano yake na wanaonekana kupuuza masomo yake.

•Akothee alionekana kudhibitisha kuwa aliwatania watu kuhusu mipango ya harusi ya pili na kuhitimu ambayo haikuwahi kutokea.

Mwanamuziki na mfanyibiashara Akothee
Image: INSTAGRAM// AKOTHEE

Mwanamuziki na mjasiriamali Esther Akoth almaarufu Akothee amewakosoa wanablogu wa Kenya kuhusu kile wanachochagua kuangazia zaidi katika maisha yake.

Katika taarifa yake siku ya Jumatano, mama huyo wa watoto watano alishangaa ni kwa nini watu wanajali sana mahusiano yake na wanaonekana kupuuza masomo yake.

Akothee alihoji ni kwa nini wanablogu wanasisitiza kufuatilia kuhusu harusi ya pili ambayo alikuwa ametangaza ingefanyika Julai lakini hakuna aliyejisumbua kumpigia simu kuhusu kuhitimu kwake ambako kulikusudiwa kufanywa Agosti 4 lakini hakukufanyika.

"Aaah kwa hivyo hakuna aliyegundua kuwa sikuhitimu Agosti 4 kama ilivyopangwa na hakuna anayeuliza kwa nini sikuwahi kuhitimu wakati kuhitimu ni jambo la umma. Na nimekuwa chuo kikuu kwa zaidi ya miaka 14. Chuo Kikuu cha Mount Kenya BBM 2013/..... Hata hivyo wanaendelea kuuliza na kufuatilia uhusiano wangu kama wengu wao,” Akothee aliandika kwenye Instagram.

Aliongeza, "Hakuna blogu inayopiga simu kuuliza kwa nini sikuhitimu kama wanavyopiga kuhusu mipango ya harusi. Hivi ndivyo unavyopima kile ambacho watu hutumia kama msukumo wa motisha au Uvumi. Mahusiano yote ni porojo, wanasubiri lini mtaachana, mtapata mimba, mfungue mtoto au mfe wakati wa kujifungua. Elimu ni motisha mara tu unapopata digrii hakuna mtu anayeweza kuiondoa."

Mwimbaji huyo mwenye umri wa miaka 43 alionekana kudhibitisha kuwa aliwatania watu kuhusu mipango ya harusi ya pili na kuhitimu ambayo haikuwahi kutokea.

“Niliwaambia hakuna harusi na hakuna graduation yote ni kiki. Mlicheswa,” alisema.

Aidha, aliendelea kuwashauri watu kuweka mahusiano yao, mafanikio na safari yao mbali na mitandao ya kijamii akionya kuwa kuna macho mabaya kila mahali.

Mapema mwezi huu, Akothee alionekana kujawa ghadhabu baada ya kuulizwa kuhusu mipango ya harusi yake ya pili na mumewe mzungu Denis 'Omosh' Shweizer ambayo iliratibiwa kufanyika Uswizi mwezi uliopita.

Chini ya moja ya machapisho yake, shabiki alimuuliza kuhusu mipango ya harusi hiyo ambayo awali alikuwa ametangaza ingefanyika Julai.

“Madam Boss hatujasahau ile harusi yako kubwa ya majuu, kwani ni lini,” mtumizi mmoja wa mtandao wa Instagram alimuuliza Akothee.

Katika jibu lake, mama huyo wa watoto watano alisema kwa utani kwamba alitengana na mume wake Denis Shweizer mara tu baada ya harusi yao ya kwanza iliyofanyika jijini Nairobi mnamo Aprili 10 mwaka huu.

Msanii huyo mwenye umri wa miaka 43 pia alitaka mwanamitandao kuangazia maisha yake mwenyewe na kusonga mbele.

"Tuliachana tarehe 11 Aprili, sasa chukua maisha yako na uendelee," alijibu.

View Comments