In Summary

•Wanyama hatimaye amevunja kimya kuhusu suala hilo alilotaja kama 'upumbavu' na kuwataka Wakenya kukoma kumhusisha na mvulana huyo wa miaka 13.

•Kwa upande mwingine, Diana alimsherehekea mtoto huyo wake wa kulea na kumhakikishia kwamba anampenda sana.

Image: INSTAGRAM// VICTOR WANYAMA

Mwanasoka wa Kimataifa wa Kenya, Victor Mugubi Wanyama amechoshwa na Wakenya kumhusisha na mwanawe mwimbaji Kelvin Bahati, Morgan Bahati.

Kwa muda mrefu, Wakenya kwenye mitandao ya kijamii wamekuwa wakimfananisha mchezaji huyo wa CF Montreal na mtoto huyo wa Bahati wa kulea na kuibua maswali mengi bila majibu.

Siku ya Jumapili, kiungo huyo wa kati mwenye umri wa miaka 32 hatimaye alivunja kimya chake kuhusu suala hilo alilotaja kama 'upumbavu' na kuwataka Wakenya kukoma kumhusisha na mvulana huyo wa miaka 13.

"Upumbavu huu unatakiwa ukome sasa!!" Wanyama alisema.

Mwanasoka huyo alieleza hisia zake kwenye mtandao wa Twitter baada ya mwanamtandao kuweka picha yake karibu na Morgan kwenye picha ya familia ya Bahati.

Kwa upande mwingine, mkewe Bahati,  Diana Marua alimsherehekea mtoto huyo wake wa kulea na kumhakikishia kwamba anampenda sana.

Mama huyo wa watoto watatu alishiriki picha yake na Morgan na akachukua fursa hiyo kujivunia ukuaji wake.

"Yule aliyeniita MUMMY kwanza. Mtoto wangu @morgan_bahati ni mzima. Mummy and son goal. Nakupenda Morgan," Diana Marua aliandika.

Mapema mwaka huu, Diana alisema ameona maendeleo na mabadiliko mengi kwa Morgan na kumtakia mwongozo wa Mungu maishani.

"Nimekuona ukibadilika na kuwa Muungwana uliye leo na kitu ninachoweza kusema ni kwamba Mungu aendelee kukulinda na aniongoze mimi na Baba yako siku zote tuweze kukulea ili uwe toleo bora kwako," alisema Januari.

Mama huyo wa watoto watatu pia alionyesha fahari yake kubwa kwa kumpa Morgan alichotaka kwa siku yake ya kuzaliwa.

Mwishoni mwa mwaka jana, Diana alijawa na fahari baada ya mwanawe huyo wa kulea kuhitimu kutoka shule ya msingi hadi Sekondari ya Chini.

Huku akimsherehekea Morgan kupitia ukurasa wake wa Instagram, Diana Marua alisema kuwa anajivunia mafanikio hayo makubwa ya mwanawe na akamhakikishia kuhusu upendo wake kwake.

"Ninajivunia kuitwa mama yako. Imekuwa ni safari na kukuona ukihitimu siku ya leo, nimeshangazwa na uaminifu wa Mungu. Nakupenda Morgan Bahati," Diana aliandika mwezi Desemba.

Mama huyo wa watoto watatu alisema hayo baada ya kuhudhuria hafla ya kuhitimu kwa watahiniwa wa darasa la sita katika Juja Preparatory School ambapo Morgan amekuwa akisomea.

Mwanamuziki Kelvin Bahati alimchukua Morgan kuwa mtoto wake mwaka wa 2014 wakati alipoenda kutumbuiza katika nyumba ya  watoto yatima ya ABC ambapo alikulia pia baada ya mama yake kuaga dunia.

View Comments