In Summary

•Shakib anaonekana kujaribu sana kujenga uhusiano mzuri na watoto wa mwanaosholaiti huyo kadiri ndoa yao inavyosonga mbele.

•Katika video hiyo, Shakib anaonekana amekaa kwenye sofa huku bintiyeTiffah  akiwa amelala mapajani mwake.

Zari Hassan, Shakib Cham, Diamond Platnumz
Image: INSTAGRAM

Ni dhahiri kwamba mume wa Zari Hassan, Shakib Cham Lutaaya anajaribu sana kujenga uhusiano mzuri na watoto wa mwanaosholaiti huyo kadiri ndoa yao inavyosonga mbele.

Siku chache tu baada ya Waganda hao kufunga pingu za maisha katika harusi nzuri ya kisasa, imeibuka video ya mfanyibiashara huyo mwenye umri wa miaka 31 akishiriki muda mzuri na binti wa pekee wa Zari, Latifah Dangote.

Katika video hiyo inayosambaa kwenye mitandao ya kijamii, Shakib anaonekana akiwa amekaa kwenye sofa huku binti huyo wa Zari na Diamond Platnumz akiwa amelala mapajani mwake. Wawili hao wanaonekana kutazama sinema kwenye Televisheni. Haijabainika ni nani alikuwa akirekodi video hiyo lakini kuna uwezekano mkubwa kuwa ni Zari mwenyewe, mtoto mwingine wa Diamond na mwanasosholaiti, Prince Nillan hata hivyo hakuonekana kwenye video hiyo.

Wanandoa hao maarufu kutoka Uganda walirasimisha ndoa yao katika harusi ya faragha iliyofanyika nchini Afrika Kusini Jumanne wiki jana. Wawili hao wamekuwa wakichumbiana kwa zaidi ya mwaka mmoja.

Maelezo ya harusi hiyo yalikuwa yamefichwa sana lakini tulifanikiwa kupata baadhi ya picha na video za sherehe hiyo ya kukata na shoka.

Picha hizo zilionyesha  Zari akiwa amevalia gauni la harusi refu jeupe huku mumewe Shakib akiwa amevalia suti ya kijivu na shati jeupe.

Wanafamilia wakiwemo watoto wa Zari; ; Pinto Tale, George Ssemwanga, Dido Ssemwanga Tiffah Dangote na Prince Nillan walikuwepo kwenye hafla hiyo. Tiffah alivalia gauni jeupe huku Nillan akiwa amevalia suti ya kijivu na shati jeupe sawa na bi na bwana harusi.

Wana wa Zari na aliyekuwa mume wake, Ivan Ssemwanga walionekana wamevalia suti nyeupe, shati jeupe na viatu vyeupe.

Wengi wa wageni waliokuwa wamealikwa kuhudhuria hafla hiyo ya faragha walionekana wamevaa mavazi meupe. Wanaume walikuwa na suti ya kijivu wakati wanawake walivaa gauni za rangi ya dhahabu.

Video inamuonyesha Shakib akisema viapo vya ndoa kisha kumvisha Zari pete kidoleni kabla ya wageni kupiga makofi kwa nguvu. Video nyingine inawaonyesha wanandoa hao wakiwa na watoto wa Zari wakipigwa picha ya familia huku wageni wakipiga makofi.

Mama yake Shakib pia alikuwepo kwenye sherehe hiyo.

Wawili hao walihalalisha muungano wao wa muda mrefu kwa mara ya kwanza katika harusi ya kidini ya Kiislamu (Nikah) mapema mwaka huu.

View Comments