In Summary

•Bahati alifichua kwamba anafanya mazoezi ya viungo katika moja ya ukumbi wa mazoezi katika eneo la Marurui, Kasarani.

•Kundi la wanamitandao liliibua wasiwasi kuhusu mwanamuziki huyo kufanya mazoezi na mkufunzi mwanamke.

Bahati akielekezwa na mkufunzi mwanamke
Image: SCREENSHOT

Siku ya Ijumaa, mwimbaji Kelvin Kioko almaarufu Bahati alifichua kwamba anafanya mazoezi ya viungo katika moja ya ukumbi wa mazoezi katika eneo la Marurui, Kasarani.

Bahati alionyesha video yake akifanya mazoezi huku mkufunzi mmoja wa kike akimwongoza kwenye kipindi hicho. Mkufunzi huyo ambaye alionekana kuwasisimua wanamitandao wengi kutokana na umbo lake la kuvutia alionekana akimpa Bahati maelekezo ya nini cha kufanya na pia kumsaidia kutumia baadhi ya vifaa.

"Mkufunzi wangu ndiye msukuma wangu. @Worldfuandi ni Motisha Yangu. Je, unapendelea mwalimu wa gym wa kiume au wa kike??" Bahati aliandika chini ya video hiyo  aliyoshiriki kwenye ukurasa wake wa Instagram.

Kama ilivyotarajiwa, mamia ya watumiaji wa mtandao wa Instagram walijitokeza kutoa maoni kuhusu video hiyo huku wengi wakionekana kumwangazia zaidi mkufunzi huyo mwanamke. Idadi nzuri ilitoa maoni kuhusu umbo zuri la mwili wake huku wengine hata wakitaka kujua uliko ukumbi huo wa mazoezi .

Kundi jingine la wanamitandao liliibua wasiwasi kuhusu mwanamuziki huyo mwenye umri wa miaka 30 kufanya mazoezi na mkufunzi mwanamke huku baadhi yao wakimuonya mkewe Diana Marua kuwa makini zaidi.

Tazama baadhi ya maoni ya wanamitandao kwenye video hiyo:-

_lilpeter Sasa hii mali baha ako nayo huku gym haitaleta confusion??

yvonne_wangare Hii Imeenda

gkserkal @diana_marua ameona hii video ama bado ako soko tuwait maneno ichemke

carolzkisilu Mama Heaven huyu usimuache aende gym peke yake aki

youngdee I love how her body is toned, she really works out

sharonnzanzika5 Diana where are you

Hata hivyo, kutokana na video hiyo, Bahati na mkufunzi walionekana kuzingatia mazoezi ya viungo tu na hakuna chochote kingine kikubwa.

Mapema mwezi huu, mkewe Bahati, Diana Marua alijivunia juhudi nyingi alizoweka katika kumsaidia kufika mahali alipo.

Kwenye Instagram, mama huyo wa watoto watatu alichapisha picha ya kumbukumbu yao na kutumia fursa hiyo kumkumbusha Bahati kuhusu jinsi alivyomtunza vizuri katika takriban miaka sita ya  ndoa yao.

"Bahati ona jinsi nilivyokutunza vizuri alafu unataka kuniaibisha hivyo kwenye video ya leo," alisema chini ya picha hizo alizopakia.

Pichani, wawili hao ambao walionekana kujawa na furaha pamoja walivalia vitenge vya bluu na maua ya rangi zingine mbalimbali. Walisimama mbele ya gari aina ya Mercedes ambayo huenda walikuwa wanatumia katika siku hizo.

Diana Marua alijibainisha kama mke bora kwa mwimbaji huyo huku akidokeza kuwa aliangukia kitu kizuri alipomuoa.

"Apataye mke mwema, anapata kitu kizuri, ni wazi, halafu ukanikopesha viatu," alisema.

Huku akijibu, Bahati alisema, "Lakini hizi ni nini ambazo unachapisha. Huyu sio mimi."

View Comments