In Summary

•Alisema kuwa Shakib alipomtembelea hivi majuzi alimwambia kwamba tayari alikuwa amefanya mipango ya harusi

• Alisema baada ya mipango ya Nikah kukamilika, mumewe walifahamisha watu wa karibu nao na wakawapatia idhini ya kuendelea.

Image: HISANI

Mwanasosholaiti maarufu wa Uganda Zari Hassan amesisitiza kwamba hakufunga ndoa (Nikah) hivi majuzi kutokana na shinikizo.

Akizungumza kwenye video ambayo alichapisha kwenye akaunti yake ya mtandao wa Snapchat, mama huyo wa watoto watano alifichua kuwa mume wake Shakib Cham Lutaaya alipanga ndoa hiyo nzima kuanzia mwaka jana.

Zari alifichua kuwa mwaka jana mpenzi huyo wake kutoka Uganda mwenye umri wa miaka 31 alidokeza kumuoa mwaka huu.

"Mwaka jana kwa utani, mume wangu alisema, 'nitakuoa mwaka ujao. Nilitengeneza video kuhusu hilo, ilikuwa snapchat," alisema.

Mfanyibiashara huyo mwenye umri wa miaka 42 alifichua kwamba Shakib alileta mada kuhusu kumuoa tena hivi majuzi tu katika msimu huu wa sikukuu ya Ramadhani wakati alipomtembelea nchini Afrika Kusini anakoishi.

Alisema kuwa Shakib alipomtembelea hivi majuzi alimwambia kwamba tayari alikuwa amefanya mipango ya harusi huku tayari akiwa amezungumza na viongozi wa kidini na wanajamii kuhusu hatua hiyo ya ndoa.

"Nilimuuliza, ngoja, umefikiria juu ya hili?" alisema.

Alisema kwamba kwa muda mfupi tu mumewe alikuwa amepanga kila kitu na viongozi wa dini  na hafla ya Nikah ikawa tayari. Alisema kuwa mambo yalifanyika haraka sana katika kipindi cha chini ya siku mbili hivi kwamba hata hakuwa na wakati wa kujiandaa na kupanga vyema kuhusu mavazi maalum ya hafla hiyo kubwa.

"Nilivaa nguo yangu na baam tulikuwa tayari kufanya harusi. Nilifanyiwa Nikah. Sio ushindani kamwe. Naishi katika nafasi yangu, nafanya mambo yangu. Nafanya yaliyo mazuri kwangu. Sio ushindani," alisema.

Mpenzi huyo wa zamani wa staa wa Bongo Diamond Platnumz alisema kuwa baada ya mipango ya Nikah kukamilika, yeye na mumewe walifahamisha watu wa karibu nao na wakawapatia idhini ya kuendelea.

"Kabla nijue, kila kitu kilikuwa kimepangwa na tukafanya Nikah. Sio kwa sababu ya shinikizo, sishindani  na yeyote," alisema.

Mama huyo wa watoto watano alibainisha kwamba ameridhika na anafurahia sana na ndoa yake na Shakib Lutaaya.

"Nipo na mume wangu kwa sababu aliamua kufanya hivyo, sio kwa mashindano, sio kwa sababu ya mtu yeyote," alisema.

Zari Hassan na Shakib walifunga ndoa ya Kiislamu almaarufu Nikkah wikendi iliyopita baada ya kuchumbiana kwa takribani mwaka mmoja.

Wawili hao walivishana pete usiku wa manane kuamkia Jumatatu katika hafla ya faraghani ambayo ilihudhuriwa na idadi ndogo ya watu.

Katika picha na video hafla hiyo iliyofanyika chumbani ambazo zilisambazwa kwenye mitandao ya kijamii, wapenzi hao walionekana wamevalia Kiislamu kabisa huku wote wakiwa wameketi kwenye mkeka uliotandikwa sakafuni.

Shakib alionekana akiinama kwa goti moja na kumvisha Zari pete ya ndoa kwa furaha kabla ya wawili hao kupigana mabusu huku watu wachache waliohudhuria hafla hiyo wakiwasherehekea kwa makofi.

Vyanzo vya habari kutoka Uganda vilidai kwamba baada ya kuvishana pete katika tukio la faraghani, wawili hao ambao wamekuwa marafiki kwa zaidi ya miaka minne waliweka Nikkah yao bayana kwa wazazi wa Zari.

View Comments