In Summary

•Madowo alisema wakati alipokuwa katika seminari, mara nyingi waliambiwa kuwa wengi waliitwa lakini walichaguliwa wachache.

•Madowo alisimulia jinsi mama yake alivyomfundisha kuhusu udadisi ulioingiana vyema na taaluma yake ya sasa; Mwandishi wa Habari.

Image: INSTAGRAM// LARRY MADOWO

Mwanahabari mashuhuri Larry Madowo alisomea ukasisi lakini hakuwahi kutawazwa.

Madowo alisema hayo alipokuwa akizungumza na kituo cha habari cha kimataifa cha CNN siku ya Alhamisi.

“Nilisomea kuwa kasisi wa Kikatoliki kwa muda mfupi. Masomo yangu yote ya sekondari nilisoma katika seminari ya Kikatoliki,” alisema.

Madowo alisema wakati alipokuwa katika seminari, mara nyingi waliambiwa kuwa wengi waliitwa lakini walichaguliwa wachache.

"Kwa hivyo nadhani mimi ni miongoni mwa wale ambao hawakuchaguliwa. Nikiwa mtoto, nilitaka kuwa mmishonari kwa sababu walisafiri ulimwenguni kote,” akasema.

"..lakini zaidi nilitaka kuwa kasisi kwa sababu nilifikiri ningeweza kuwasaidia watu. Bado ninasaidia watu kama mwandishi wa habari, lakini kwa njia tofauti."

Madowo alisimulia jinsi mama yake alivyomfundisha kuhusu udadisi ulioingiana vyema na taaluma yake ya sasa; Mwandishi wa Habari.

“Mama yangu alikuwa mwalimu wa shule ya msingi ambaye alinifundisha udadisi, ukarimu na heshima. Alihakikisha kuwa nimesoma vitabu na kumfanyia muhtasari,” alisema.

"Alikuwa na redio ili mimi na dada yangu tuweze kusikia habari kutoka kila kona ya dunia. Baba yangu alileta magazeti nyumbani kila siku, nami nikayasoma.”

Madowo alisema wazazi wake wote wawili walipanda mbegu ya uandishi wa habari ndani yake, ingawa hawakuishi muda mrefu wa kuiona ikiota na kumea.

"Nadhani kukua katika maeneo ya mashambani nchini Kenya kulifungua macho yangu kwa ukandamizaji na ukosefu wa haki, na kila mara ninahakikisha kwamba hadithi zangu hazizingatii matajiri na wenye nguvu isivyofaa. Uandishi wa habari una nguvu zaidi unapofanya kazi kwa maslahi ya umma,” alisema.

Madowo alifanya kazi miaka 10 kwenye televisheni nchini Kenya.  Anasema ameitwa msaliti kwa kutangaza habari za Kiafrika kwenye vyombo vya habari vya Kimataifa vya CNN.

Madowo alisema kwa kuwa amekaa muongo mmoja kwenye runinga ya Kenya, watu hujibu simu zake na mara nyingi watu wanamtumia mawazo ya kile anachopaswa kuangazia.

"Ingawa watu wengine wanajivunia kuniona kwenye CNN, wengine wanatarajia niwe "mzalendo" kwa kuonyesha tu upande mzuri wa Kenya na Afrika," alisema.

"Kuna watu wanaohisi kudharauliwa wanapomwona Mwafrika mwenzao akizungumzia jambo lisilopendeza kuhusu bara, na nimeitwa msaliti mara nyingi."

Madowo alisema anaona kazi yake ni kueleza ukweli usiofichuliwa kuhusu bara hili, na sio kuwa mwanasiasa wa Afrika kwenye jukwaa la kimataifa.

"Nadhani ninaleta mtazamo muhimu katika utangazaji wa CNN wa Afrika kama mtu ambaye alizaliwa na kukulia katika bara," alisema.

"Natumai kuwa utaalam wangu wa ndani na sarafu yangu ya kitamaduni itasaidia kuelezea mtazamo wa pande tatu wa hadithi ninazoandika."

View Comments