In Summary

• Pritty Vishy alikuwa mmoja wa wale waliosafiri kutoka Nairobi kuhudhuria mazishi ya mwanaharakati huyo.

• Alifika akitarajia kuwaona wengi wa LGBTQ lakini akapigwa butwaa kwa kutoona hata mmoja.

Pritty Vishy awasuta wanaLGBTQ kwa kutohudhuria mazishi ya Chiloba
Image: Instagram

Mwanablogu Pritty Vishy amewakandia watu ambao walikuwa wanamuomboleza aliyekuwa mwanaharakati wa LGBTQ Edwin Kiprotich Kiprop almaarufu Chiloba huku wakijitambulisha kuwa wanachama wenza.

Vishy ambaye pia alidokeza kuwa alisafiri hadi Elgeyo marakwet kuhudhuria hafla ya mazishi ya mwanaharakati huyo aliyeuawa katika mzozo wa kimapenzi na mpenzi wake wa kiume Jackton Odhiambo, alisikitishwa sana kuona hakuna mwanachama wa LGBTQ hata mmoja alijitokeza kumpa buriani mwenzao, licha ya kuupiga mwingi kwenye mitandao ya kijamii kuonesha jinsi walikuwa wanamkubali kama mwanaharakati wao.

Vishy aliwasuta wanachama wote wa LGBTQ na kuwaambia kuwa walimuaibisha mwenzao na kumtoroka katika kifo chake, huku akisema hakuna haja wajijaze mitandaoni kumuomboleza na siku ya mazishi wote waingie mitini.

Aliwataka kuanzia leo kufyata ndimi zao.

“Wakati nilisafiri kuhudhuria hafla ya mazishi ya Chiloba, nilikuwa natarajia kuwaona wale wote ambao walikuwa wanajiita marafiki na familia kwa Chiloba. Lakini nilichokina kilikuwa kinyume na matarajio yangu. Mbona walikuwa wanapiga mdomo huku na kule… kumbe mnaongea vile mlimpenda au vile mnampenda lakini hamkutokea kumsindikiza. Bure kabisa, mnyamaze na muache mbwembwe,” Pritty Vishy alisema.

Chiloba alizikwa Jumanne baada ya kutolewa mochwari siku hiyo hiyo na taarifa za ndani zinasema kuwa hakuna rafiki yake kutoka wale wote waliokuwa wakimuomboleza mitandaoni kama mwenzao wa LGBTQ.

Jumatano kumekuwa na mjadala mkali iwapo mtu anaweza jitokeza kuhudhuria msiba wa rafiki yake au siku hizi kumesalia ni kuonesha mapenzi mitandaoni ikifika siku yenyewe kila mtu anajishughulisha na hamsini zake.

 

View Comments