In Summary

• Ishara ya kuachana kwao inakuja wiki kadhaa tu baada ya kutangaza kutarajia mtoto wa kwanza pamoja kama wapenzi.

• Rapudo alimvisha Ray pete ya uchumba mwishoni mwa mwaka jana jijini Dubai.

Kennedy Rapudo na mpenzi wake Amber Ray
Image: Instagram

Kennedy Rapudo, mchumba wa mwanamitindo Amber Ray ameendelea kuibua maswali mengi kuliko majibu kwa wanamitandao ambao wanahisi uhusiano wao umegonga mwamba.

Wapenzi hao wawili waliovishana pete za uchumba mwishoni mwa mwaka jana jijini Dubai hivi majuzi ilibainika kwamba kila mmoja ameacha kumfuata mwenzake kwenye mtandao wa Instagram ambako walipenda sana kumiminiana sifa.

Za hivi punde ni kwamba Rapudo amefuta picha zote za Amber Ray ambazo alikuwa amepakia kweney ukurasa wake wa Instagram huku akiachia ujumbe wenye ukakasi kwenye instastory yake – kiashiria kwamba huenda mambo si mazuri katika uhusiano wao.

Katika ujumbe huo ambao wengi wameitafsiri kama ufafanuzi wa vitendo vya kufuta picha na kuacha kufuatana Instagram, Rapudo anasema wakati mwingine kuendelea kung’ang’ania jambo kunaleta madhara makubwa kuliko kuliachia liende vile linaenda tu.

Ikumbukwe Rapudo na Ray walikuwa wanachumbiana hapo nyuma baada ya mwanasosholaiti huyo kuachana na mchezaji wa mpira wa vikapu kutoka Sierra Leone, IB Kabaa.

Baada ya wiki kadhaa, Ray alidokeza kuachana na Rapudo lakini tena wakarudiana, safari hii kwa mapenzi motomoto hadi kuvishana pete za uchumba katika hafla ya kifahari.

Walikuja wakatangazia wanamitandao kuwa hatimaye wanatarajia mtoto pamoja, Ray akimpa koja la maua Rapudo kwamba ndiye mtu wa kipekee aliyefanya uamuzi wa kubeba ujauzito wake.

Sasa haijulikana kama pia wameachana hata baada ya kumpokea mtoto wao au ni kiki tu wanafukuzia mitandaoni kwa kufuta picha zao na kuacha kufuatana!

Uhusiano wao ulikuwa umeanza kushabikiwa kwa jinsi walikuwa wanashirikiana kuwalea watoto ambao kila mmoja aliingia kwenye uhusiano huo na mtoto wake.

View Comments