In Summary

• "Promota wamekataa kuafikiana na makubaliano ya awali…” sehemu ya taarifa ya Diamond

Diamond asitisha shoo yake Ujerumani, Promota aingia mitini.
Image: Instagram

Msanii Diamond Platnumz ametangaza kusitishwa kwa shoo yake ambayo alikuwa anatarajiwa kutumbuiza nchini Ujerumani jiji la Berlin Jumamosi.

Msanii huyo alikuwa anatarajiwa kutumbuiza katika shoo ya Afro Fest 2023 katika ukumbi wa Verti Music Hall.

Kulingana na taarifa ambayo Diamond aliitoa Jumamosi jioni, saa chache tu kuelekea muda mwafaka wa kutinga ukumbini, alimlaumu promota wa shoo hiyo kwa kukiuka makubaliano na hivyo kuifanya iwe vigumu kwa msanii huyo kupanda jukwaani.

“Tangazo kwenu mashabiki wa Diamond Platnumz, tunasikitishwa kuwataarifu kwamba sitoweza kutumbuiza kwenye tamasha la Afro Fest Berlin kwa sababu promota wamekataa kuafikiana na makubaliano ya awali…” sehemu ya taarifa ya Diamond ilisoma.

Msanii huyo aliwaomba radhi mashabiki wake wa huko Ujerumani kwa kuwaangusha kwani si kupenda kwake bali ni visingiti ambavyo viko nje ya uwezo wake.

“Najua taarifa hii itawavunja moyo wengi na tunaomba msamaha kwa mapungufu yote ambayo taarifa hii huenda imezua. Hata hivyo bado tunaendelea kuwa na majadiliano na promota ili tulipige jambo hili pasi haraka iwezekanavyo. Ahsante sana kwa kuwa waelewa,” Diamond alitoa taarifa.

Msanii huyo alikuwa anarejea nchini Ujerumani kwa mara ya pili chini ya mwaka mmoja, ambapo mara ya kwanza alikuwa huko mwaka jana alikwenda kwa ajili ya kuitambulisha na kuiuza albamu yake ya FOA ambapo ilipata mafanikio makubwa barani Ulaya, lakini pia kufanya mahojiano  ambapo alifunguka mengi kuhusu safari yake ya muziki na kwa nini hataku kuingia katika ndoa wakati ambapo anaendelea na muziki.

View Comments