In Summary

•Ghetto Kids walikuwa wamewafurahisha majaji na kupata ufuasi mkubwa nchini Uingereza na Afrika nzima.

• Kundi hilo awali liliweza kusherehekewa na waimbaji  wa Marekani  P. Diddy na Nicki Minaj.

Wapiga densi kutoka Uganda Ghetto kids.
Image: INSTAGRAM

Wapiga densi kutoka Uganda wanaofahamika kama Ghetto Kids walichujwa katika fainali za Britain Got Talent Usiku wa Jumapili, mei 5.

Watoto hao ambao wengi  wao ni mayatima waliwakilisha nchi ya Uganda katika mashindano hayo na walikuwa wamewafurahisha majaji na kupata ufuasi mkubwa nchini Uingereza na Afrika nzima.

Washindi hao wa tuzo za AFRIMMA katika kitengo cha densi bora Afrika waliweza kuingia nusu fainali za Britain Got Talent baada ya Jaji Bruno Tonioli kuwapa Golden Buzzer katikati ya onyesho lao.

Hii ilikuwa mara ya kwanza katika historia ya maonyesho hayo kwa wawaniaji kupata Golden Buzzer kabla ya kukamilisha onyesho lao.

Kundi hilo awali liliweza kusherehekewa na waimbaji  wa Marekani  P. Diddy na Nicki Minaj, na mwaka wa 2017, kundi hilo lilishiriki kwenye wimbo wa  Unforgettable wake French Montana, huu ukiwa mwanzo wa  mafanikio yao nchini Marekani.

Mnamo Januari 2023, Ghetto Kids walisafiri hadi Ufaransa kutumbuiza wakati wa mapumziko wakati wa mchezo wa nyumbani wa klabu ya soka ya Paris Saint-Germain(PSG) dhidi ya Reims kwenye Uwanja wa Parc des Princes.

Kabla ya mechi hiyo kuanza watoto hao walikutana na wachezaji wa PSG kama vile Kylian Mbappé.

Kikundi hicho kina jumla ya watoto 30.

Wameshinda tuzo kadhaa zikiwemo AFRIMMA ya densi Bora ya Afrika mwaka 2017, BEFFTA ya Crew Bora ya densi mwaka 2016, Tuzo za HIPPO za Trailblazer mwaka 2015, PAFA ya Kundi Bora la Mitindo mwaka 2017, AEA - USA kwa Kundi Bora la densi  mwaka 2017. , Tuzo za RIAA Marekani (2017), na Tuzo za Watayarishi wa YouTube (2020).

View Comments