In Summary

Kwa kudhamini kitendo cha uadilifu na uungwana wake, Mutua aliongeza pesa zingine zaidi na kumtumia yule jamaa.

• Watu walimmiminia sifa Mutua lakini pia jamaa huyo ambaye Mutua hata hivyo hakumtaja kwa jina wala jinsia.

Ezekiel Mutua abaki hoi baada ya mtu kumrudishia pesa alizomtumia kimakosa.
Image: Facebook

Mkurugenzi mkuu mtendaji wa MCSK Ezekiel Mutua amesimulia kisa ambacho kilimtokea na ambacho kilimuacha kufikiria sana kuwa kumbe kuna salio la watu wazuri bado duniani.

Mutua kupitia ukurasa wake wa Facebook alielezea jinsi alijipata ametuma hela shilingi elfu 5 kwa namba ya mtu tofauti na yule aliyekuwa anataka kutumia.

Kwa haraka, Mutua alianzisha mchakato wa kutuma ombi kwa wahudumu wa M-Pesa kurudisha hizo hela lakini kabla hajatuma ombi hilo, alipokea ujumbe kutoka kwa jamaa yule ambaye alikuwa ametumia pesa kimakosa.

Ujumbe wenyewe uliuwa wa kumshukuru Mutua kwa kumtoa shimoni, katika kile alisema kuwa alikuwa amefika mwisho na Mutua alikuja kwake kama mwokozi aliyetumwa na Mungu licha ya kuwa hawajuani.

“Nilitumia mtu 5k kimakosa. Nilipogundua nilianza mara moja mchakato wa kuzirudisha na Safaricom lakini nilipata ujumbe kutoka kwa mpokeaji kunishukuru kwa mpesa, akisema kwamba alikuwa katika hali mbaya na alikuwa ameomba muujiza,” Mutua alisema.

Mutua alibung’aa na kushindwa cha kusema, alimjibu huyo jamaa akimwambia kwamba pesa hizo alizipokea kimakosa na kumtaka arudishe.

Mpokeaji alipita mtihani huo kutoka kwa Mutua na kurudisha hela hizo zote, ishara ambayo ilimshangaza hata Zaidi Mutua kwani jamaa yule aliweza kuwa na ujasiri wa kurudisha licha ya kudai kwamba alikuwa hana chochote mbele nyuma.

Kwa kudhamini kitendo cha uadilifu na uungwana wake, Mutua aliongeza pesa zingine zaidi na kumtumia yule jamaa kama shukrani kwa kuonesha uaminifu.

“Nilimwambia kwamba nilikuwa nimemtumia pesa kimakosa na nikaomba wabadilishe muamala huo. Alifanya hivyo na nikaiongeza na kuirudisha kwao. Alifaulu mtihani wa uadilifu aliporudisha pesa na hakuanza kufanya biashara ya tumbili. Kiasi cha kwanza nilichotuma kwake kilikuwa kimakosa. Ya pili ilikuwa muujiza. Uadilifu unalipa!” Mutua alimaliza kwa furaha.

Watu walimmiminia sifa Mutua lakini pia jamaa huyo ambaye Mutua hata hivyo hakumtaja kwa jina wala jinsia.

View Comments