In Summary

• Msanii huyo ameonekana kubadilisha msimamo wake kuhusu mapenzi, ikiwa ni miezi kadhaa baada ya kujitokeza akikiri wazi mapenzi yake kwa Ringtone.

Justina Syokau asema hataki mapenzi
Image: Instagram

Justina Syokau amewalilia watu ambao hawataki kumpa kazi kwa kuhofia kwamba anaweza enda kazini mwao na kuiba wanaume wao.

Katika video ambayo aliifanya na kuipakia kwenye TikTok YAKE, Justina Syokau alilia akisema kwamba maisha yake yamekwama kwa sababu ya kutopata kazi za kufanya kupitia muziki wake.

Msanii huyo wa ‘2020’ alisema kwamba wengi wamekuwa wakimnyima kazi kwenye hafla na matamasha yao tangu alipodanganya kuwa amefanyiwa upasuaji wa kuongeza makalio.

Syokau aliwatoa wasiwasi akisema kwamba yeye hajawahi na hawezi kumchukua mume wa mtu, huku akisema kuwa hana haja na ndoa tena kwani aliumizwa vibaya katika ndoa yake ya awali.

“Kwa wale hamtaki kunipea kazi kwenye matamasha za kutumbuiza, wengine nasikia wanasema eti ooh Justina atakuja na hayo makali yake kubwa kwa event yangu anichukulie bwana, mimi huwa sina shughuli na bwana wa mtu, sijawahi hata kuchumbiana mwanaume aliyeoa,” Justina alijitetea.

“Hata sijawahi fikiria kuchumbiana na mume wa mtu, hata mwenyewe sina hamu ya mapenzi na marafiki zangu wanaonijua watakwambia sina shughuli na ndoa tena, niliumizwa kwa ndoa yangu sana. Niliumizwa sana na siwezi enda tena kwa ndoa nyingine. Mwenyewe hata mtu akinikatia namtukana na wengine hata nawablock... kwa sababu mapenzi yalinitenda,” aliongeza.

Msanii huyo ameonekana kubadilisha msimamo wake kuhusu mapenzi, ikiwa ni miezi kadhaa baada ya kujitokeza akikiri wazi mapenzi yake kwa msanii wa injili mwenye kashfa nyingi, Ringtone Apoko.

Justina alipoweka makalio ya kughushi, alisema kwamba alifanya vile kama njia moja ya kuwavutia wanaume wa kumtongoza na kumuoa. Hii ni baada ya Ringtone kuonekana kutoonyesha kukubali kwake kuhusu Syokau kumtaka kimapenzi.

Katika ufunuo wake kwenye video hiyo ya dakika kumi, Syokau ameonekana kufutilia mbali mambo mengi ikiwemo muziki wake ambao ameuita kama ucheshi, makalio bandia lakini pia mapenzi.

Anachokitaka kwa sasa, na ambacho alikisisitiza ni kupata kazi ili mambo yake yaweze kurudi kwenye barabara kuu baada ya kuingia kwenye mtaro katika miezi ya hivi karibuni, akisema kuwa hata mwanawe pia ni mgonjwa na anahitaji huduma za kiafya – ambazo zinahitaji mfuko pia.

 

View Comments