In Summary

• “Umekuwa ni wakati mgumu sana, miezi kadhaa iliyopita nimepitia moto na kusema ukweli nimeona mkono wa Mungu,” aliongeza.

Jackie Matubia
Image: Screengrab//YouTube

Muigizaji wa zamani katika kipindi cha Zora, Jackie Matubia alizidiwa na hisia za uchungu wakati anasimulia kwamba amekuwa akiwalea mabinti zake peke yake pasi na kusaidiwa na baba zao.

Matubia alisema haya katika podikasti kwenye chaneli yake ya YouTube ambayo alizungumzia kwa undani kilichomfanya kuondoka katika uhusiano wake na muiizaji huyo mwenzake waliyekutana kwenye kipindi hicho kilichokamilika mapema mwaka jana.

Mama huyo wa mabinti wawili kutoka kwa baba tofauti alizua dhana kwamba Blessing Lung’aho hawajibiki katika kumsaidia kulea binti yao baada ya kuachana miezi michache iliyopita.

Matubia alisisitiza kwamba maisha yake tangu kuachana na Lung’aho hayajakuwa rahisi na kwamba ni Mungu tu amekuwa akimshikilia muda wote.

“Mungu kwa kweli amekuwa katika kitovu cha maisha yetu, mimi na mabinti zangu, amenishikilia sana wakati kila kitu katika maisha yangu kilikuwa kinasambaratika. Mungu alinishika mkono na kunipa hakikisho kwamba yeye ni Alfa na Omega. Amekuwa baba kwa wanangu na amekuwa nguzo ya kuegemea,” Matubia alisema.

“Umekuwa ni wakati mgumu sana, miezi kadhaa iliyopita nimepitia moto na kusema ukweli nimeona mkono wa Mungu,” aliongeza.

Matubia na Lung’aho waliachana miezi kadhaa iliyopita kwa mtindo wa kimya kimya bila ya mmoja wao kujitokeza na kuzungumza kama wako pamoja au la.

Hata hivyo, katika siku za hivi karibuni, Matubia ameonekana kujitokeza na kumwaga mtama kwa kuku wengi, akitoa ubuyu kuhusu kile kilichotokea kati yao na kutia sumu kwenye asali ya penzi lao.

View Comments