In Summary

• Edday Nderitu, ambaye aliigura ndoa yake mwaka jana na kuondoka zake kwenda Marekani pamoja na watoto wote alikuwa anasherehekea siku yake ya kuzaliwa, Mei 22.

Samidoh na Edday Nderitu
Image: HISANI

Afisa wa polisi ambaye pia ni msanii wa nyimbo za Kikuyu, Mugithi, Samidoh amekuwa gumzo kwenye mitandao ya kijamii kwa mara nyingine tena baada ya kuchukua hatua ya kumtakia heri njema za siku ya kuzaliwa mkewe, Edday Nderitu.

Kupitia insta story yake, Samidoh alipakia picha ya mama wanawe 3 na kuiambatanisha na ujumbe mzuri, akimsherehekea kama mwanamke mwenye ushawishi mkubwa katika maisha yake.

Edday Nderitu, ambaye aliigura ndoa yake mwaka jana na kuondoka zake kwenda Marekani pamoja na watoto wote alikuwa anasherehekea siku yake ya kuzaliwa, Mei 22.

Katika ujumbe wake, Samidoh alimsherehekea Edday Nderitu kama mama wa kizazi chake akimkumbuka kwa kumbuumbu za jinsi walikuwa wanacheka pamoja na kufanya mambo makubwa kabla ya ndoa yao kuyumba.

“Tunasherehekea furaha tele ya mama mtukufu wa kizazi chetu kwenye Siku yake ya Kuzaliwa. Hii ni siku ya kuzaliwa iliyojaa vicheko, kumbukumbu za pamoja, na urafiki wa kudumu. Hbd Edday Nderitu,” Samidoh aliandika.

Ikumbukwe wakati anaondoka, Edday Nderitu alidokeza kwamba hali haikuwa nzuri katika ndoa yake ya miaka 15 na Samidoh, akisema kwamba katu asingevumilia kuwalea wanawe katika penzi linalohusisha wake wawili kwa mume mmoja.

Hii ni baada ya Samidoh kurudiana tena na mama wanawe, seneta Karen Nyamu ambaye pia uhusiano wao kwa muda uikuwa ni wa kifaurongo – leo upo, kesho haupo!

Nderitu baadae aliwaingiza wanawe katika mfumo wa masomo nchini Marekani na kufichua kwamba sababu kubwa ya kuondoka nao wote kutoka humu nchini ni kwa ajili ya kulinda maslahi ya akili zao, haswa binti kifungua mimba ambaye alikuwa amefika umri wa utineja.

Mama huyo wa watoto watatu alisema kwamba alilenga kumlinda mwanawe kisaikolojia ili asije kushuhudia machafuko katika mzozo wa ndoa ya wazazi wake, kwani alikuwa amefikia umri wa kujitambua.

View Comments