In Summary

•Wawili hao walionekana wakisherehekea baada ya Ufaransa kufunga penalti ya mwisho kuthibitisha ushindi wao mkubwa.

•Pogba alitambua uwepo wa Diamond kwa kutazama mchuano huo na alipongeza sapoti yake kwa Ufaransa katika Euro 2024.

Image: HISANI

Staa wa Bongofleva, Naseeb Abdul Juma almaarufu Diamond Platnumz alipata bahati ya kutazama mechi ya Ufaransa dhidi ya Ureno Ijumaa usiku pamoja na kiungo wa zamani wa Ufaransa Paul Pogba.

Mastaa hao wawili ambao kwa sasa wako Dubai walionekana wakifurahia muda pamoja katika burudani huku wakifuatilia mechi hiyo ya robo fainali ya Euro 2024. Walishuhudia Ufaransa wakiwachapa Ureno katika mikwaju ya penalti na kufuzu kwa hatua ya nusu fainali.

Katika video iliyochapishwa kwenye Instagram, walionekana wakisherehekea baada ya Ufaransa kufunga penalti ya mwisho kuthibitisha ushindi wao mkubwa.

"Wakati wa sherehe kwa Ufaransa @paulpogba @diamondplatnumz," maelezo kwenye video hiyo yalisomeka.

Mara baada ya mchezo huo kumalizika, Pogba alionekana akisimama na kushangilia kabla ya kuanza kupiga densi huku wimbo wa Rhumbaukicheza.

Kiungo huyo wa zamani wa Man United na Juventus alitambua uwepo wa Diamond kwa kutazama mchuano huo na alipongeza sapoti yake kwa Ufaransa katika Euro 2024.

“Nipo hapa na kaka yangu. Alikuja kusapoti timu. Amevaa blue, yeye ni wa blue,” Pogba alisema kwenye video aliyoichukua akiwa na Diamond.

Diamond pia alieleza furaha yake kwa Ufaransa kushinda mechi hiyo ya robo fainali na kueleza imani yake kuwa timu hiyo ingeshinda hata kombe la Euro 2024. .

“Wafaransa wangu tumeshinda!!! Niamini kombe ni letu,” alisema.

Kwa sasa, Diamond yuko nchini Dubai kwa ziara ya kikazi huku Pogba akiwa nchini humo kwa ajili ya kujivonjari.

Pogba kwa sasa anatumikia marufuku ya miaka minne ya kutoshiriki shughuli za kandanda baada ya kupatikana na hatia ya matumizi ya dawa za kusisimua viungo.

View Comments