In Summary

•Takriban miezi saba iliyopita Ghost aliandamana na kakake kuelekea India ili kumtolea figo moja baada ya vipimo vya daktari  vilivyofanyika hapa nchini kubaini marehemu alihitaji figo nyingine.

•Mtangazaji mwenza Gidi Ogidi ameandika ujumbe wake wa rambi rambi huku akiombea familia ya Ghost nguvu za kupambana na majonzi.

Ghost Mulee na marehemu kakake Mike
Image: INSTAGRAM// GHOST MULEE

Mtangazaji wa kipindi cha Gidi na Ghost asubuhi Jacob 'Ghost' Mulee yuko katika hali ya kuomboleza.

Kocha huyo wa zamani wa timu ya taifa Harambee Stars amempoteza kakake Mike ambaye alikuwa na uhusiano wa karibu mno naye.

Ghost alitumia ukurasa wake wa Instagram kutangaza habari hizo za kusikitisha huku akimtaja kakake kama rafiki, shabiki na mshauri wake mkubwa.

"Mike ndugu yangu umepigana vita vizuri. Bwana akupe kibali mpaka tukutane tena!" Ghost aliandika.

"Safiri salama ndugu yangu rafiki yangu shabiki wangu mshauri wangu! Mungu anaweza!" Aliandika.

Mamia ya wanamitandao ikiwemo mashabiki na watu mashuhuri wamejumuika mitandaoni kumfariji Ghost katika kipindi hiki cha majonzi.

Mtangazaji mwenza Gidi Ogidi ameandika ujumbe wake wa rambi rambi huku akiombea familia ya Ghost nguvu za kupambana na majonzi.

"Ghost Mulee, nimekuona ukisimama na kaka yako kwa zaidi ya miezi 6. Haijawa rahisi. Pole sana kaka. Acha Mike apumzike na Mwenyezi akufariji wewe na familia," Gidi  aliandika.

Takriban miezi saba iliyopita Ghost aliandamana na kakake kuelekea India ili kumtolea figo moja baada ya vipimo vya daktari  vilivyofanyika hapa nchini kubaini marehemu alihitaji figo nyingine.

Hata  hivyo walipofika India upasuaji wa kubadilisha figo haukufanyika kwani  mtaalamu aliyekuwa anahudumia marehemu alipata figo yake kuwa sawa na akasema sio lazima.

Sote hapa Radio Jambo tunaungana na Ghost katika kuomboleza huku tukiomba Mola afariji  familia  yake na kuipa nguvu ya kukabiliana na majonzi katika kipindi hiki kigumu.

View Comments