In Summary

• Rais Trump alikuwa amedai kuwepo kwa udanganyifu katika upigaji kura.

• Ofisi ya utawala wa huduma za serikali imesema inamtambua Bwana Biden kama "mshindi".

• Jumatatu, Bwana Biden alizindua timu itakayoangazia sera ya fedha na usalama wa taifa.

Rais mteule Joe Biden Kushoto na rais Trump kulia

Donald Trump amekubali kuanza kwa mchakato rasmi wa kumkabidhi madaraka Rais mteule Joe Biden.

Rais amelitaka shirika linaloshughulikia mabadilishano hayo "lifanye kile kinachostahili kufanywa", hata wakati anaahidi kuendelea kupinga matokeo.

Ofisi ya utawala wa huduma za serikali imesema inamtambua Bwana Biden kama "mshindi".

Hilo linawadia wakati Bwana Biden ameidhinishwa rasmi kama mshindi wa jimbo la Michigan na kuwa pigo kubwa kwa Trump.

Rais mteule Joe Biden, PICHA: REUTERS

Timu ya Bwana Biden imefurahishwa na kuanza kwa mchakato huo wakati rais mteule anajiandaa katika sherehe za kuapishwa Januari 20.

"Uamuzi wa leo ni hatua iliyohitajika kuanza kukabiliana na changamoto zinazokumba taifa letu ikiwemo kudhibiti ugonjwa wa virusi vya corona na kuboresha uchumi tena," taarifa iliyotolewa imesema.

"Uamuzi huo ni hatua ya kiutawala ya kuanza rasmi kwa mchakato wa mabadilishano ya madaraka na mashirika husika."

Mapema Jumatatu, Bwana Biden alizindua timu itakayoangazia sera ya fedha na usalama wa taifa iliyojumuisha watu wa zamani wa miaka hiyo katika utawala wa Obama.

Biden atamchagua Anthony Blinken kuwa waziri wa mambo ya nje na John Kerry kama mjumbe wa masuala ya mabadiliko ya tabia nchi, huku Janet Yellen ikidokezwa kwamba ndiye atakayekuwa mwanamke wa kwanza kuwa waziri wa fedha.

Trump alisema nini?

Trump aliandika ujumbe kwenye mtandao wa Twitter wakati ofisi ya utawala wa huduma za serikali ambayo ndiyo yenye jukumu rasmi la kuanza mchakato wa mabadilishano ya madaraka inaarifu timu ya Biden kwamba itaanza mchakato huo.

Afisa wa ofisi hiyo Emily Murphy alisema dola milioni 6.3 sawa na (£4.7m) amezitenga kwa ajili ya rais mteule.

Wakati anaahidi kuendelea na "vita hivyo muhimu", rais alisema: "Haidhuru, kwa maslahi ya nchi yetu, Napendekeza Emily na timu yake kufaya kile kinachostahili kwa kuzingatia itifaki za awali na pia nimearifu timu yangu kufanya vivyo hivyo."

Bi. Murphy, aliyeteuliwa na Trump alitaja "matukio ya hivi karibuni ya kisheria yanayopinga matokeo ya uchaguzi" katika uamuzi wake wa kutuma burua hiyo.

Amesema hajapokea shinikizo lolote kutoka Ikulu ya Marekani kwa muda ambao ametoa uamuzi wake.

"Kuwa wazi, sikupokea maagizo yoyote ya kuchelewa kufanya uamuzi wangu," Barua ya Murphy kwa Biden imesema.

"Lakini nilipokea vitisho kwa njia ya mtandao na barua pepe vilivyoelekezwa kwa usalama wangu, familia yangu, wafanyakazi wangu na hata wanyama wangu wa nyumbani kushinikiza kufanya uamuzi huu mapema.

"Hata wakati nakabiliwa na vitisho elfu kadhaa nimeendeelea kuhakikisha sheria inafuatwa."

Murphy alikosolewa na pande zote za kisiasa kwa kushindwa kuanza mchakato wa mabadilishano ya madaraka mapema ambao kawaida huwa ni kati ya kipindi cha uchaguzi na hafla ya kuapishwa.

Bi. Murphy alishindwa kufikia siku ya ukomo ya Jumatatu ya kuanza shughuli hiyo iliyokuwa imetengwa na wabunge wa chama cha Democratic katika bunge la wawakilishi kuwaarifu wabunge hao kuhusu kuchelewa kuanza kwa shughuli hiyo.

 

Je wabunge wa Republican walitoa shinikizo lolote?

Wabunge wa chama cha Trump cha Republican wamekuwa wakiendelea kuzungumza kuhusu shughuli ya mabadilishano ya madaraka siku za hivi karibuni wengi wakijitokeza siku ya Jumatatu.

Seneta wa Tennessee Lamar Alexander, ambaye anastaafu, alitoa taarifa akisema kuwa Trump anastahili "kutoa kipaumbele kwa nchi" na kumsaidia Biden kuchukua usukani.

"Maisha yako yakiwa yanamwilikwa na umma, watu hukumbuka kitu cha mwisho ulichofanya," Bwana Alexander alisema.

Rais Donald Trump, Picha: GETTY IMAGES

Seneta wa West Virginia Magharibi Shelley Moore Capito alisema "inafika wakati, uchaguzi wa mwaka 2020 lazima ufike mwisho".

Seneta Bill Cassidy wa Louisiana alisema timu ya sheria ya Trump legal imeshindwa kutoa ushahidi wa madai ya wizi wa kura wanayodai ulikumba uchaguzi, na kuongeza kuwa mabadilishano "yanastahili kuanza kwa ajili ya taifa hilo".

BBC

View Comments