In Summary

•Stevo alikuwa mgeni katika shoo ya Bustani la Massawe, ambapo alizungumzia mambo mbalimbali kuhusu maisha yake.

•“Kupika pia, ndio kama nimetoka shoo kama nimechoka, lazima mke aandalie mume wake chakula," alisema Stevo.

Stevo Simple Boy ndani ya studio za Radio Jambo.
Image: RADIO JAMBO

Rapa maarufu wa Kenya Stephen Otieno Adera almaarufu Stevo Simple Boy ametangaza wazi kwamba hayuko kwenye uhusiano wowote kwa sasa.

Mwimbaji huyo wa kibao ‘Freshi Barida’ ndiye aliyekuwa mgeni  wa siku ya Jumanne katika shoo ya Bustani la Massawe na Valentine Ludiema, ambapo alizungumzia mambo mbalimbali kuhusu maisha yake.

Katika mahojiano hayo, alifichua kuwa kwa sasa anatafuta mwanamke ambaye atakuwa mke bora kwake.

“Wanadada wapo, lakini tunaangalia yule ako sahihi. Awe na heshima, awe Mcha Mungu, alafu pia aniheshimu na awe mwenye bidii. Sio eti anakuja kwangu kwa sababu mimi maarufu sana,” Stevo Simple Boy alisema.

Mwanamuziki huyo aliongeza, “Kupika pia, ndio kama nimetoka shoo kama nimechoka, lazima mke aandalie mume wake chakula.”

Stevo pia alikanusha madai kuwa yeye ni mchekeshaji, akisisitiza kuwa yeye ni msanii anayefanya muziki. Pia alikiri kwamba kupata mialiko ya maonyesho haijakuwa rahisi kwani baadhi ya watu wanafikiri hajakomaa kimuziki.

Miezi kadhaa iliyopita, tetesi ziliibuka kuwa ndoa ya Stevo ilikuwa kwenye mtafaruku baada ya kudaiwa kuumizwa moyo na aliyekuwa mkewe, Grace Atieno.

Kuliibuka uvumi mwingi usiothibitishwa kuwa mwanamuziki huyo na aliyekuwa mkewe, Grace Atieno walikuwa wakikumbwa na matatizo katika ndoa yao baada ya rapa huyo kugundua kuwa ana ujauzito wa mwanaume mwingine.

Simple Boy alimtambulisha Grace Atieno kama mke wake halisi hadharani wakati wa hafla ya mazishi ya babake mnamo Februari 11 mwaka jana.

"Bwana asifiwe. Kwa majina mimi ni Stephen Otieno. Mimi ndiye kitinda mimba wa Anthony Adera, na huyu ndiye mke wangu," alisema mwimbaji huyo kabla ya kumpa kipaza sauti mke wake mrembo aliyesimama kando yake.

Baada ya kupokea kipaza sauti, Bi Atieno alimwomboleza baba mkwewe huku akionyesha wazi wazi ukaribu uliokuwepo kati yake na marehemu.

"Bwana asifiwe. Kwa majina ni Grace Atieno. Nimeoleka kwa Bwana Stephen Otieno. Naskia vibaya kumpoteza mtu mwenye alikuwa akinitoa kila wakati..." Grace alisema kabla ya kuzidiwa na hisia na kuangua kilio.

Kwenye mahojiano ya mwaka jana, Stivo aliweka wazi kwamba alikuwa anaishi na mke huyo wake wa zamani jijini Nairobi. Aliweka wazi kwamba yeye na Grace wanapendana sana na wanapanga kuendeleza mahusiano yao.

Hata hivyo, alibainisha kwamba bado hawajabarikiwa na mtoto pamoja.

Stivo aliachana na mtumbuizaji Pritty Vishy mapema mwaka wa 2022, miezi michache tu baada ya uhusiano wao kujulikana hadharani.

Wawili hao hata hivyo ilidaiwa hawakuwahi kuwa na uhusiano wa kimapenzi kwani Stivo alidaiwa kutaka kusubiri ndoa kabla ya kushiriki tendo la ndoa na mtumbuizaji huyo mwenye umri wa miaka 21.

View Comments