"Nimepoteza kilo 33" mwanamuziki King Kaka afunguka kuhusu ugonjwa ambao umemwathiri kwa miezi mitatu

King Kaka amefichua kuwa hajakuwa na hisia ya ladha kwa kipindi cha miezi miwili na amekuwa akila matunda na kunywa uji tu

Muhtasari

•Msanii huyo anayefahamika sana kwa kibao chake 'Wajinga nyinyi' amesema kuwa tangu aanze kuugua amepoteza kilo 33 na kiuno chake kimepungua na inchi tatu

•Kaka amesema kuwa hata nguo alizokuwa anavaa hapo awali hazimtoshei kwa sasa kufuatia kupungua kwa ukubwa wa kiuno chake.

Image: INSTAGRAM// KING KAKA

Mwanamuziki tajika nchini Kennedy Ombima almaarufu kama King Kaka ametoa ombi kwa mashabiki wake kumkumbuka katika maombi yao akisema kwamba amekuwa akiugua kwa kipindi cha miezi mitatu na siku nane ambacho kimepita.

Kupitia kurasa zake za mitandao ya kijamii, King Kaka amefichua kuwa hajakuwa na hisia ya ladha kwa kipindi cha miezi miwili na amekuwa akila matunda na kunywa uji tu.

Msanii huyo anayefahamika sana kwa kibao chake 'Wajinga nyinyi' amesema kuwa tangu aanze kuugua amepoteza kilo 33 na kiuno chake kimepungua na inchi tatu.

" Mashabiki wangu, nimeona ni heri niwaambie haya. Nimekuwa mgonjwa kwa miezi mitatu na siku nane. Nilipimwa vibaya. Nimepoteza kilo 33 kwa wakati huo na tulianza kutembea hospitalini. Nimefanyiwa vipimo vyote na hakuna matokeo. Cha kushangaza ni kuwa sina maumivu yoyote na tunatumai kuwa tutapata suluhu hivi karibuni. Kiuno changu kilikuwa na ukubwa wa 36 na sasa ni 33" King Kaka aliandika.

Kaka amesema kuwa hata nguo alizokuwa anavaa hapo awali hazimtoshei kwa sasa kufuatia kupungua kwa ukubwa wa kiuno chake.

Hata hivyo ameeleza kuwa ana matumaini ya kupata nafuu hivi karibuni kuona kuwa alianza kula chakula takriban wiki tatu zilizopita

"Nilikuwa nanywa uji na kula matunda kidogo. Nilianza kula chakula wiki tatu zilizopita na polepole nitazoea. Sijakuwa na hisia ya ladha kwa miezi miwili" Amesema Kaka.

Msanii huyo amewashukuru Mungu kwa uhai na marafiki wote ambao wamekuwa wakimjulia hali tangu aanze kuugua.

King Kaka amesema kwamba anawapeza sana watoto wake na akashukuru mkewe Nana Owiti pamoja mama yake ambao wamekuwa wakimsaidia katika safari yake ya matibabu. 

"Napeza watoto wangu, mke wangu @nanaowiti amekuwa nguzo langu kwa hiyo mitatu pamoja na mamangu. Ninachotaka kwenu ni maombi tu hakuna kingine" Kaka aliandika.

Amesema kuwa ana matumaini ya kupona kwani alizaliwa kuwa mshindi.