Babake Jahmby Koikai afichua jambo maalum marehemu aliwaambia usiku ambao alikufa

Mzazi wa Jahmby Koikai amefunguka kuhusu matukio maalum ya mwisho na marehemu bintiye.

Muhtasari

•Katika ujumbe wake, Njambi ambaye alikuwa hospitalini wakati huo alitoa shukrani zake kwa babake na kumwambia baadhi ya vitu vya kumnunulia.

•Bw Koikai pia alizungumza kuhusu ujumbe maalum ambao binti yake alimpa yeye na mzazi mwenzake Bi Stella Wambui usiku alipofariki.

amezungumzia matukio maalum na bintiye Njambi Koikai.
Bw Daniel Koikai amezungumzia matukio maalum na bintiye Njambi Koikai.
Image: HISANI

Bw Daniel Koikai, babake marehemu Mary Njambi Koikai almaarufu Jahmby Koikai amefunguka kuhusu matukio maalum ya mwisho na bintiye marehemu.

Huku akimuomboleza bintiye katika ratiba ya hafla ya mazishi iliyofikia Radio Jambo, Bw Koikai alitoa maelezo kuhusu uhusiano wake na marehemu bintiye.

Alitaja uhusiano wao kuwa na nyakati nzuri na mbaya, ingawa walikutana tu wakati Njambi alipokuwa shule ya upili kwani alikuwa akifanya kazi nje ya nchi wakati wa utoto wa binti yake.

Wakati ulipokuwa mzuri, tulikuwa tukienda kununua vitu na kula chakula cha mchana kwenye baadhi ya mikahawa jijini, na ulifurahia kukutana nami sana. Ninakosa sana nyakati nzuri tulizoshiriki pamoja.

Wakati tulipokuwa na uhusiano mbaya, zingepita siku au miezi kadhaa bila kuzungumza, jambo ambalo najilaumu na nitafanya hivyo kila mara kwani nimepoteza nafasi ya kurekebisha hali na wewe,” Bw Koikai aliandika.

Mfanyibiashara huyo aliendelea kufichua ujumbe ambao binti yake alimtumia siku moja tu kabla ya kufa.

Katika ujumbe wake, Njambi ambaye alikuwa hospitalini wakati huo alitoa shukrani zake kwa babake na kumwambia baadhi ya vitu vya kumnunulia.

“Haya baba, natumai umefika nyumbani salama. Kwa hivyo ningehitaji beri nyekundu ya maji ya machungwa kutoka Del Monte na juisi safi ya machungwa na nyanya ya mti. Madaktari wapo hivyo itabidi niende tukaongee kesho. Ilikuwa nzuri kukuona na kuungana tena,” ujumbe wa Njambi kwa baba yake ulisomeka.

Bw Koikai pia alizungumza kuhusu ujumbe maalum ambao binti yake alimpa yeye na mzazi mwenzake Bi Stella Wambui usiku alipofariki.

Marehemu Njambi aliwaambia wazazi wake kuhusu umoja na kuthamini uwepo wa baba yake.

"Huko hospitalini karibu na kitanda chako na mama yako, usiku ulipotuacha, uliniambia sisi ni damu moja na unafurahiya kuwa nimekuja. Tuliungana tena na natumai tutaungana tena siku moja,” Bw Koikai alifichua.

Babake Njambi aliitaka roho ya bintiye kupumzika kwa amani ya milele.