Video ya mwimbaji Vybz Kartel na mpenziwe baada ya kutoka gerezani yazua wasiwasi (+video)

Uso wake umeonekana kuwa umevimba kwenye mashavu, jambo linaloonyesha wazi kwamba afya yake si nzuri sana.

Muhtasari

•Vybz ameoyesha picha na video kadhaa zake akiwa nje ya gereza na akishiriki nyakati nzuri na marafiki na wanafamilia wake.

•Pia alionekana akiwa ameshika chupa ya kileo huku akijirekodi na mpenzi wake na kumsifia .

Image: HISANI

Msanii maarufu wa dancehall kutoka Jamaika, Adidja Palmer, almaarufu Vybz Kartel hatimaye amekuwa mtu huru.

Mwimbaji huyo aliachiliwa kufuatia uamuzi wa mahakama wa Jumatano alasiri, ambapo iliamuliwa kwamba yeye na wenzake hawapaswi kushtakiwa tena.

Katika kurasa zake za mitandao ya kijamii, mwanamuziki huyo mwenye umri wa miaka 48 ameendelea kuwashirikisha mashabiki wake kuhusu kuachiliwa kwake. Ameoyesha picha na video kadhaa zake akiwa nje ya gereza na akishiriki nyakati nzuri na marafiki na wanafamilia wake.

Katika mojawapo ya video alizochapisha ambayo imezua mjadala mkubwa mtandaoni, alionekana kwenye gari na mpenzi wake, Sidem Ozturk. Pia alionekana akiwa ameshika chupa ya kileo huku akijirekodi na mpenzi wake na kumsifia .

“Nimetoka! Mimi na mke wangu,” Vybz Kartel alisema kwenye video hiyo.

Katika video hiyo, staa a huyo wa dancehall alikuwa amefunika kichwa chake. Hata hivyo, mtu angeweza kuona kwamba ana uso wake umevimba kwenye mashavu, jambo linaloonyesha wazi kwamba afya yake si nzuri sana.

Wanamitandao wameendelea kutoa hisia mseto kufuatia video hiyo,baadhi wakizungumzia afya yake, wengine wakizungumza kuhusu uhusiano wake, huku wengine wakisherehekea kuachiliwa kwake.

Tazama maoni kutoka kwa baadhi ya wanamtandao;

Dk Jay: Bosi wa Dunia!  Tafadhali acha pombe na uchukue virutubisho vya NAD+, Maji ya Nazi na Dawa zote za udongo ili kujenga afya!💪 Dunia tayari ni yako! Karibu tena! Afya ni Utajiri.

Decapro: Unaugua nini, uponyaji wa haraka kutoka kwa asili, na uhuishaji. Kenya inasubiri ziara yako.

Fanya Mema: Yooo Vybz kwa kweli unaonekana mgonjwa, uso umevimba, umepauka sana

Jayson A. Rivera, Esq: Mke atakuwa na ujauzito kufikia jana.

Albert Nat Hyde: Miaka 12 ya maisha yako imepita!

Tweezy: Miaka 12 haikuwa nzuri kwake.. Karibu nyumbani.

Jumatano alasiri, mahakama ya rufaa ya Jamaica ilitoa uamuzi dhidi ya kusikilizwa tena kwa kesi hiyo, ikitaja sababu mbalimbali ikiwa ni pamoja na utovu wa nidhamu wa baraza la waamuzi na kuzorota kwa afya ya msanii huyo.

Mahakama ya Rufaa, ikiongozwa na Jaji Marva McDonald-Bishop, iliamua kwa kauli moja kuwaachilia Vybz Kartel na washtakiwa wenzake, Shawn ‘Shawn Storm’ Campbell, Andre St John, na Kahira Jones.

"Kwa kuzingatia masuala yote ambayo mahakama imezingatia, tunahitimisha kwamba maslahi ya haki hayahitaji kesi mpya kuamriwa kwa wakata rufaa," alisema Jaji Marva McDonald-Bishop.

 "Kwa hiyo tunatoa amri ifuatayo: hukumu na uamuzi wa kuachiliwa huingizwa kuhusiana na wakata rufaa," aliongeza.