logo

NOW ON AIR

Listen in Live

Zari Amkikingia Kifua Shakib Dhidi Ya Wanaokejeli Kiingereza Chake Kwenye Netflix

“Mume wangu ataonekana kwenye Netflix, lakini wewe hapo na Kiingereza chako kizuri, jiangalie!” Zari aling’aka.

image
na MOSES SAGWEjournalist

Burudani14 January 2025 - 08:53

Muhtasari


  • Alimshauri mfanyibiashara huyo wa nguo kutoka Uganda kutokwazwa na maneno ya watu mitandaoni, na kumtaka siku zote kuzikita mbona zake kwenye zawadi kuu ya kutafuta hela. 
  • “Sijawahi mpenda mtu mwingine kama ambavyo nimempenda Shakib na kuona nyota yake iking’aa hivi,” Zari aliongeza.



MFANYIBIASHARA Zari Hassan amejitokeza na kufoka vikali dhidi ya watumizi wa mitandao ya kijamii wanaokejeli na kukosoa Kiingereza cha mumewe, Shakib Cham Lutaaya.


Zari na Shakib ni miongoni mwa mastaa waliojumuishwa kwenye msimu wa tatu wa kipindi cha uhalisia cha Young, Famous & African kwenye jukwaa la utiririshaji la Netflix.


Kionjo cha kipindi hicho ambacho kitapeperushwa Januari 17 kilichapishwa mitandaoni wiki iliyopita na watumizi wa mitandao ya kijamii haswa kutoka Afrika Mashariki walikuwa wa haraka kukejeli Kiingereza cha Mganda huyo.


Hata hivyo, Zari ameamua kuvunja kimya na kunyoosha mtutu wa bunduki ya maneno kwa wakosoaji hao akisema kwamba wataishia tu kukosoa Kiingereza kibaya cha mumewe mitandaoni lakini yeye tayari ameshafanikiwa kuingia kwenye jukwaa hilo kubw zaidi la kutiririsha video.


“Eti ooh, hatutangoja kuona na kusikia Kiingereza cha SHAKIB… achene sasa tuzungumze kuhusu hicho Kiingereza. Acha tuzungumze! Acha niwaambie kitu, huu umekuwa ni msimu wa ushindi kwa mume wangu. Kwa kunioa, mume wangu aliangukia na huu umekuwa msimu wake wa kuvuna pakubwa,” Zari alisisitiza.


“Mume wangu ataonekana kwenye Netflix, lakini wewe hapo na Kiingereza chako kizuri, chenye lafudhi ya kuvutia na ujuzi wa kipekee,  jiangalie! Mume wangu anaenda kuonekana kwenye jukwaa kubwa zaidi duniani la video – Netflix, na wewe utashinda hapo. Hata hujihurumii!” Zari aliwapalia makaa wakosoaji.


Mama huyo wa watoto watano alizidi kumvisha koja la maua mume wake akisema kwamba hata alijizolea umaarufu maradufu kumliko baada ya kuonekana naye kwenye Netflix.


Alimshauri mfanyibiashara huyo wa nguo kutoka Uganda kutokwazwa na maneno ya watu mitandaoni, na kumtaka siku zote kuzikita mbona zake kwenye zawadi kuu ya kutafuta hela.


“Na kupitia kuonekana kwenye Netflix, si siri kwamba dili kubwa zitabisha sasa. Nani anayejua, pengine mume wangu hata atanipita na pengine kufika Hollywood. Mpenzi wangu usiyumbishwe, na kwenu nyinyi mabibi na mabwana, huu ni msimu wa ushindi kwa Shakib. Nina furaha kubwa kwake.”


“Sijawahi mpenda mtu mwingine kama ambavyo nimempenda Shakib na kuona nyota yake iking’aa hivi,” Zari aliongeza.


Hii ni mara ya kwanza kwa Shakib kutokea kwenye kipindi hicho kwani msimu wa kwanza na wa pili miaka miwili iliyopita, Zari aliigiza na aliyekuwa mumewe, Diamond Platnumz.



RADIO JAMBO FREQUENCIES

Kisumu 100.1 | Mombasa 92.3 | Nakuru 96.9 | Eldoret 99.5 | Nyeri 99.3 | Nyahururu 97.3 | Webuye 95.3 | Meru 92.7 | Kitui 104.9 | Kibwezi 104.7 | Voi 105.7 | Malindi 98.1 | Lamu 104.7 | Narok 97.3 | Kapenguria 99.7 | Kisii 89.3 | Garissa 104.3 | Maralal 97.3 | Lodwar 92.7


logo© Radio Jambo 2024. All rights reserved