
Mwanahabari mkongwe wa Kenya Leonard Mambo Mbotela amefariki dunia.
Mkwe wake Anne Mbotela alithibitisha habari hizo za kusikitisha kwa Radio Jambo Ijumaa asubuhi.
Mwanahabari huyo mkongwe alikuwa hajisikii vizuri kwa muda na alikata roho mwendo wa saa tatu unusu asubuhi siku ya Ijumaa.
"Ni kweli baba mkwe wangu amefariki," Anne alisema.
Mbotela alikuwa amemuoa Alice Mwikali ambao kwa pamoja walipata watoto watatu: Aida Mbotela, Jimmy Mbotela na George Mbotela.
Mwanahabari huyo nguli alisifika kwa kipindi chake maarufu cha redio na TV kilichoitwa Jee Huuu ni Ungwana kilichopeperushwa kwenye redio na TV za KBC.
Programu hiyo iliundwa mnamo 1966 na ilifurahia kupeperushwa kwa takriban miaka 55.