Harmonize ashindwa kujizuia jukwaani, afunguka mapenzi yake kwa ex wa Diamond, Hamisa akitumbuiza

"Sijali italeta shida, hii ni serious lakini. Hakuna haja ya kuficha hisia zangu tena. Ninampenda sana,” Harmonize alikiri.

Muhtasari

•Wakati akitumbuiza wikendi, Harmonize alimwaga ya moyoni na kukiri mapenzi yake makubwa kwa mama huyo wa watoto wawili.

•Mara baada ya kukiri hisia zake, mashabiki walianza kuimba jina la Hamisa kumuonyesha sapoti mwimbaji huyo.

Harmonize na Hamisa Mobetto
Image: INSTAGRAM

Staa wa Bongo, Rajab Abdul Kahali almaarufu Harmonize ameendelea kufunguka kuhusu hisia zake kwa mwanamitindo Hamisa Mobetto.

Wikendi, bosi huyo wa Konde Music Worldwide alipokuwa jukwaani akiwatumbuiza mashabiki wake katika tamasha alitumia nafasi hiyo kumwaga ya moyoni na kukiri mapenzi yake makubwa kwa mama huyo wa watoto wawili.

Alionekana akimsifia mpenzi huyo wa zamani wa Diamond Platnumz na kukiri kuwa hisia zake za mapenzi kwake ni za dhati kabisa.

“Naona inafaa kuwaambia jinsi ninavyompenda Hamisa Mobetto. Hii ni serious. Sijali italeta shida, hii ni serious lakini. Hakuna haja ya kuficha hisia zangu tena. Ninampenda sana,” Konde Boy aliwaambia mashabiki wake.

Mara baada ya kukiri hisia zake, mashabiki waliojitokeza kwa ajili ya shoo hiyo walianza kuimba jina la Hamisa Mobetto kumuonyesha sapoti mwimbaji huyo.

Haijabainika iwapo Harmonize anatania tu au anavutiwa kweli na mwanamitindo huyo mrembo ambaye tayari yupo kwenye huba nzito na Mtogo Kevin Sowax.

Wakati alipoulizwa kuhusu Harmonize kukiri wazi kumpenda, Hamisa alisisitiza kuwa tayari yuko kwenye mahusiano dhabiti akidokeza kwamba hakuna uwezekano wa yeye kukubali ombi la mwimbaji huyo kuwa mpango wake wa kando.

"Sina cha kujibu lakini kumbukeni jamani mimi ni mke wa mtu, shemeji yenu yaani anaupiga mwingi,” Hamisa Mobetto alijibu wiki iliyopita wakati wa kipindi cha moja kwa moja kwenye mtandao wa Instagram.

Mapema mwezi jana, Harmonize alimsihi mwanamitindo Hamisa ampe nafasi moyoni mwake licha ya kuwa kwenye mahusiano mengine.

Bosi huyo wa Konde Music Worldwide aliachia wimbo ambapo alimwambia mpenzi huyo wa zamani wa Diamond kwamba yuko tayari kuwa mpango wake wa kando. Ingawa hakutaja jina lake waziwazi katika wimbo huo, ungeweza kujua wazi kwamba maneno hayo yalielekezwa kwa mama huyo wa watoto wawili.

Katika wimbo huo, mwimbaji huyo anamwambia Hamisa Mobetto anafahamu fika kwamba ana mpenzi lakini anamsihi kutoruhusu uhusiano wake na Mtogo Kevin Sowax usimnyime nafasi katika maisha yake.

"Sijui kama ni wakati mwafaka wa kusema hivi. Ninachojua ni kwamba sina budi kukuambia hili. Umbo lako la mwili linanifanya nifanye hivi. Je, unaona? Mpenzi natumai unajua hili. Najua una mwanaume. Unaonekana unaenda kuwa mke wa mtu. Naweza kuwa mtu wako bora. Usinipoteze, nifanye tu mpango wako wa kando,” Konde Boy anaimba katika wimbo huo ambao aliachia mwishoni mwa wiki iliyopita.

 Anaendelea, "Je, huoni sura yako nzuri kwenye wallpaper yangu? Hiyo ina maana niko tayari kukupa karatasi yangu yote (Baby karatasi yangu yote). Acha niwe mpango wako wa kando (x5). Nataka kuwa mpango wako wa kando. Mpenzi nifanye kuwa mpango wako wa kando. Naapa nasubiri hadi uwe wangu."