Mwana wa rais wa Uganda ambaye pia ni jenerali wa jeshi la watu wa Uganda (UPDF) Muhoozi Kainerugaba, amefunga akaunti yake ya X awali twitter siku chache baada ya kukiri kuwa angemng’oa kiongozi wa upinzani wa nchi hiyo Bobi Wine kichwa chake.
Hatua ya mkuu huyo wa jeshi la Uganda limesababisha gumzo mtandaoni ikizingatiwa alikuwa na Zaidi ya wafuasi milioni moja kwenye jukwaa hilo la kijamii mtandaoni.
Kulingana na chapisho lake la la mwisho kwenye anwani yake ya X, mwana huyo wa rais Yoweri Kaguta Museveni alisema kwamba ameamua kuondoka kwenye ‘vichochoro vya mtandao huo’ kwa kuitikia mwito wa Yesu Kristo wa kumataka kuweka makini yake yote kwa jeshi la Uganda.
Akaunti ya Muhoozi yenye zaidi ya wafuasi milioni moja ilifunguliwa mwaka wa 2014.
“Hata hivyo, wakati umefika sasa chini ya maagizo na baraka za Bwana wangu Yesu Kristo kuondoka na kujikita katika jeshi lake, UPDF.” Sehemu ya ujumbe wa mwisho wa Muhoozi kwenye ukurasa wake wa X, ulisema.
Hata hivyo, kiongozi huyo aliyekuwa na hisia tata kwenye jukwaa la X, ameelezea Imani kuwa wafuasi wake watazidi kumfuatilia hata nje ya X, akifahamu kuwa wafuasi wanaomfuata wanampenda mno.
Aidha mwanajeshi huyo mwenye cheo cha juu zaidi katika UPDF ameashiria kuwa atarudi kwenye jukwaa hilo katika siku za usoni Mungu akiruhusu baada ya kumaliza kazi yake ya kurejesha amani ya kudumu kwa watu wake.
Kwenye ujumbe huo, jenerali Muhoozi alimalizia akisema
kwamba sapoti izidishwe kwa taifa la Uganda na Afrika kwa jumla sawia na kwa
baba wake aliyemtaja kuwa rais wa mapinduzi.