'Peleka mtoto kwa babake apate baraka' - wanawake waambiwa

Mchungaji huyo alidai kuwa hakuna mwanamke yeyote ana mamlaka ya kubariki mtoto.

Muhtasari

•Mchungaji Elizabeth Mokoro amewashauri wanawake kuwapeleka watoto kwa baba yao ili kupokea baraka.

•Mchungaji huyo alidai hata kama mahusiano yalisambaratika sharti mwanamke apeleke mtoto kwa babake

MCHUNGAJI ELIZABETH MOKORO
MCHUNGAJI ELIZABETH MOKORO
Image: SCREENGRAB

Mchungaji Elizabeth Mokoro wa kanisa la Seventh Day Adventist  amewashauri wanawake wanaowazuia watoto kukutana na kuwajua baba zao baada ya kuvunjika kwa  mahusiano.

Kwa mujibu wa Mokoro,watoto siku zote watakutana na baba zao siku moja na hivyo wanawake wanapaswa kuacha kudanganya watoto kwamba baba zao wamekufa ilhali wako hai.

'Una mtoto na najua baba yake alikuumiza lakini acha kuwadanganya kwamba baba yake alikufa.Siku moja watakutana.' Mchungaji Mokoro alisema.

Hata hivyo ,mchungaji huyo alielezea kuwa yeye hakupokea baraka kutoka kwa baba mzazi japo anawashauri wanawake kupeleka watoto kwa baba yao.

'Wengine wetu hatukupokea baraka kutoka kwa baba zetu.Mama yako alikulea hivo,lakini nenda  ukafungamane na baba yako .Tafuta baba yako.' Mokoro alishauri.

Mchungaji huyo aliendelea kwa kusema kuwa hakuna mwanamke yeyote ambaye ana mamlaka ya aina yoyote ile kubariki mttoto wake.

'Hakuna mwanamke ambaye ana mamlaka ya kubariki mtoto.Hakuna!' Mchungaji Mokoro alisema.

Wiki chache zilizopita,kanisa la seventh adventist church lilibatilisha uamuzi wake wa kuwasimamisha kazi viongozi wanne wa kidini katika mimbari zao.

Mabadiliko haya yalikuja kufuatia mabishano makubwa ya mtandaoni na malalamiko ya umma kufuatia kusimamishwa kwa awali.

Mchungaji Elizabeth Mokoro, Kenneth Maina, Mwinjilisti Shaban Ndege, Mwinjilisti Millicent Odhiambo, na Mwinjilisti Lantena walikuwa miongoni mwa watu waliopangiwa kufutwa kazi.

Mnamo Julai 4, SDA Kenya Field Coast ilitoa notisi ya kuwakataza watu hawa kuhudumu katika matawi yao. Agizo hilo lililotiwa saini na katibu mtendaji mchungaji Eliab Ombuoro liliwaagiza washiriki wa kanisa kutowapa viongozi hao fursa zozote za kuhudumu ndani na nje ya eneo la SDA Kenya Coast.