BARABARA YA ATWOLI

Mwanaharakati Boniface Mwangi aapa kuangusha tena ishara ya barabara ya Atwoli

Atwoli alitangaza kuwa camera za CCTV ziliwekwa ili kulinda usalama wa eneo hilo baada ya ishara hiyo kuwekwa tena.

Muhtasari

•Ishara ya barabara ya Atwoli iliwekwa tena baada ya kupatikana imeangushwa asubuhi ya kuamkia Jumapili

•Wakili Ahmednasir Abdullahi aliahidi Mwangi kumwakilisha mahakani iwapo atakamatwa kwa kuangusha ishara hiyo.

Ishara ya 'Francis Atwoli Road' ilipatikana imeanguka Ijumaa
Ishara ya 'Francis Atwoli Road' ilipatikana imeanguka Ijumaa
Image: HISANI

Mwanaharakati Boniface Mwangi ametishia kuangusha tena ishara ya barabara ya 'Francis Atwoli Road' iliyowekwa na serikali ya kaunti ya Nairobi upande wa Kileleshwa siku ya Ijumaa.

Hii ni baada ya ishara hiyo kuwekwa tena baada ya kupatikana imeangushwa asubuhi ya kuamkia Jumapili na mtu asiyetambulikana.

"Nilitoka kwa tumbo ya mwanamke jasiri. Kama bado ishara hiyo itakuwa nitakaporejea nyumbani, nitaiangusha mimi mwenyewe." Mwangi aliandika kwenye akaunti yake ya Twitter.

Kwa sasa Mwangi yuko nchini Luxembourg ambapo alipokezwa tuzo la 'Luxembourg Peace Prize'

Mwangi pia aliwasihi wakazi wa eneo la Dik Dik kuangusha ishara ile huku akiwaambia kuwa wakikosa kuiangusha watoto wao wangeadhirika na kile alichoita 'Atwolisis'(kuiga tabia na mienendo ya Atwoli).

Kikundi kikubwa cha wanamitandao kilionekana kupongeza aliyeangusha ishara hiyo huku wengine wakiagiza iangushwe tena baada ya kuwekwa kwa mara ya pili.

"Uharibifu ni kutokujali na ni jambo lililopitwa na wakati katika nchi inayoamini kuwa kuna sheria na mikakati ya kufuatwa ikiwa hujaridhika. Sipendelei machafuko. Hata hivyo,maafisa wa polisi wanachunguza tendo hilo" katibu mkuu wa COTU, Francis Atwoli aliandika kwenye mtandao wa Twitter baada ya kuona picha ya ishara hiyo ikiwa imelala chini.

Hata hivyo, baadae siku hiyo Atwoli alitangaza kuwa ishara ile ilikuwa imewekwa tena na serikali ya Kaunti na camera za upelelezaji almaarufu kama CCTV zikawekwa ili kulinda eneo hilo.

"Serikali ya Kaunti ya Nairobi imeweka tena ishara ya barabara iliyoangushwa . Ikiwa unafikiria ulitoka kwa mwezi, nenda ukaiangushe tena. Pia camera za CCTV zimewekwa ili kulinda eneo ile" Atwoli aliandika.

Tangazo hilo la Atwoli ndilo lililomfanya mwanaharakati Boniface Mwangi kutangaza kuwa angeangusha ishara ile pindi atakaporudi Kenya.

Wakili Ahmednasir Abdullahialmaaarufu kama 'Grand Muller'  aliahidi Mwangi kumwakilisha mahakani iwapo atakamatwa kwa kuangusha ishara hiyo.

"Ukikamatwa kimakosa wakati unatekeleza wajibu tukufu wa kuondoa hicho kidonda cha macho mtaani, basi nitakutafutia wakili  ama nilipe malipo ya kuwakilishwa na wakili ama mimi mwenyewe nikuwakilishe.. chaguo ni lako" Grand Muller alimwambia Mwangi.