logo

NOW ON AIR

Listen in Live

Barasa awachiliwa kwa dhamana ya 100,000 baada ya kukanusha mashtaka ya kushambulia mwanakandarasi

Barasa kwa upande wake alidai kuwa madai dhidi yake ni vita ya kisiasa ambayo inatekelezwa  na  mahasidi wake kwenye siasa.

image
na Radio Jambo

Yanayojiri03 August 2021 - 02:21

Muhtasari


•Licha ya kurekodiwa akimzaba kofi mwanakandarasi huyo na video hiyo kuenezwa sana mitandaoni, Barasa alikanusha mashtaka ya kushambulia Masinde mbele ya mahakama.

•Mbunge huyo ambaye ni mwandani wa naibu rais William Ruto alikamatwa na maafisa wa polisi kutoka kituo cha Kimilili Jumatatu asubuhi akiwa nyumbani kwake maeneo ya Nasianda.

•Kesi hiyo itaendelea mnamo Septemba 27.

Didmus Barasa mahakamani siku ya Jumatatu

Habari na John Nalianya

Mnamo Jumatatu mbunge wa Kimilili Didmus Barasa alifikishwa mahakamani kusomewa mashtaka  dhidi yake ya kusababisha majeraha  mabaya mwilini wa mwanakandarasi Stephen Wekesa Masinde.

Licha ya kurekodiwa akimzaba kofi mwanakandarasi huyo na video hiyo kuenezwa sana mitandaoni, Barasa alikanusha mashtaka ya kushambulia Masinde mbele ya mahakama.

Mwanasiasa huyo pamoja na wengine ambao hawakuwa pale mahakamani wanadaiwa kumsababishia Masinde majeraha mabaya mwilini mnamo Julai 30 walipokuwa katika shule ya msingi ya Lurare Baptist.

Mbunge huyo ambaye ni mwandani wa naibu rais William Ruto alikamatwa na maafisa wa polisi kutoka kituo cha Kimilili Jumatatu asubuhi akiwa nyumbani kwake maeneo ya Nasianda.

Hakimu Gladys Odhiambo alimuachilia mwanasiasa huyo kwa dhamana ya shilingi 100,000 baada yake kukanusha mashtaka.

Kesi hiyo itaendelea mnamo Septemba 27.

Wakili wa mlalamishi Brian Khaemba alipongeza polisi kwa kumkamata Barasa kwa upesi na kutaka haki kutendeka.

Khaemba alisema kuwa mahakamana ilikuwa imeagiza Barasa kutomtishia mlalamishi ambaye pia ni mwanamuziki tajika maeneo ya Magharibi mwa Kenya. 

"Tumewasilisha ombi la kutaka kesi hii kuhamishwa kutoka hapa Kimilili na kupelekwa kwa korti ingine nje ya eneo bunge hili. Hivo mteja wangu ambaye si mwenyeji wa hapa atakuwa salama na huru kuendelea na kesi" Wakili alisema. 

Barasa kwa upande wake alidai kuwa madai dhidi yake ni vita ya kisiasa ambayo inatekelezwa  na  mahasidi wake kwenye siasa.


RADIO JAMBO FREQUENCIES

Kisumu 100.1 | Mombasa 92.3 | Nakuru 96.9 | Eldoret 99.5 | Nyeri 99.3 | Nyahururu 97.3 | Webuye 95.3 | Meru 92.7 | Kitui 104.9 | Kibwezi 104.7 | Voi 105.7 | Malindi 98.1 | Lamu 104.7 | Narok 97.3 | Kapenguria 99.7 | Kisii 89.3 | Garissa 104.3 | Maralal 97.3 | Lodwar 92.7


logo© Radio Jambo 2024. All rights reserved