logo

NOW ON AIR

Listen in Live

Maelfu ya wanandoa wapya Zimbabwe wagundua vyeti vyao vya ndoa ni batili

Wanasheria pia walionya ikiwa una cheti batili huwezi kupata talaka.

image
na Samuel Maina

Habari24 March 2024 - 05:25

Muhtasari


  • •Imeibuka kuwa, kwa sababu ya suala la ukarani, vyeti vilivyotolewa ndani ya miezi 18 iliyopita ni batili.
  • •Wanasheria pia walionya ikiwa una cheti batili huwezi kupata talaka.

Maelfu ya waliooana hivi karibuni nchini Zimbabwe wameshangaa kujua kwamba vyeti vyao vya ndoa si halali.

Imeibuka kuwa, kwa sababu ya suala la ukarani, vyeti vilivyotolewa ndani ya miezi 18 iliyopita ni batili, ugunduzi ambao unaweza kuathiri wanandoa wote waliofunga ndoa ndani ya kipindi hiki.

Jambo hilo lilikuja kujulikana wakati Chama cha Wanasheria cha Zimbabwe kilitoa notisi ya tahadhari kwa wanasheria kote nchini.

Kilibainisha kuwa vifaa vya kuandikia vinavyotumika kwenye vyeti vya ndoa vya kiraia vinaendelea kunukuu sura ya sheria ya zamani ya ndoa ambayo ilibatilishwa mnamo mwaka 2022.

Sheria mpya, ambayo ilianza kutumika Septemba 2022, ilileta mabadiliko makubwa, ikiwa ni pamoja na haki kwa wapenzi katika ndoa za kitamaduni. Pia iliharamisha ndoa za utotoni.

Chama cha wanasheria kimewashauri walioathirika kupeleka vyeti vyao kwa msajili ambaye atarekebisha na kugonga muhuri wa hati hiyo.

Wanasheria pia walionya ikiwa una cheti batili huwezi kupata talaka.

Wapenzi kadhaa waliooana hivi karibuni ambao walizungumza na BBC hawakujua hapo awali kwamba vyeti vyao vinaweza kuwa batili.

Mkanganyiko huo uliibua gumzo kwenye majukwaa mbalimbali ya mitandao ya kijamii, huku wengine wakitania ilikuwa fursa kwa wale wanaotafuta njia ya kutoka nje ya ndoa zao.

Idara ya Usajili wa Kiraia iliambia jarida linalomilikiwa na serikali The Chronicle kwamba ingawa inaweza kurekebisha vyeti vilivyopo, haiwezi kuchapisha maandishi mapya yenye sheria sahihi bila serikali kwanza kutangaza mabadiliko hayo kupitia gazeti la serikali.


RADIO JAMBO FREQUENCIES

Kisumu 100.1 | Mombasa 92.3 | Nakuru 96.9 | Eldoret 99.5 | Nyeri 99.3 | Nyahururu 97.3 | Webuye 95.3 | Meru 92.7 | Kitui 104.9 | Kibwezi 104.7 | Voi 105.7 | Malindi 98.1 | Lamu 104.7 | Narok 97.3 | Kapenguria 99.7 | Kisii 89.3 | Garissa 104.3 | Maralal 97.3 | Lodwar 92.7


logo© Radio Jambo 2024. All rights reserved