logo

NOW ON AIR

Listen in Live

Uganda ilishirikiana na Kenya kumkamata Besigye Nairobi – Waziri wa ICT Uganda

Waziri huyo Chris Baryomunsi alisema Serikali ya Uganda ilikuwa inawasiliana na serikali ya Kenya kabla ya kukamatwa kwa Besigye.

image
na Davis Ojiambo

Habari22 November 2024 - 15:23

Muhtasari


  • Usemi huu unakinzana na wa PS wa mambo ya nje wa Kenya Dkt. Korir SingOei kuwa mamlaka nchini Kenya haikufahamu kukamatwa na kusafirishwa kwa Besigye.


Waziri wa ICT na Mwongozo wa Kitaifa wa Uganda Chris Baryomunsi amesema serikali ya Kenya ilifahamu na ilishiriki katika kukamatwa kwa kiongozi wa upinzani Kizza Besigye jijini Nairobi.

Matamshi ya waziri huyo wa Uganda yanakinzana na yale ya katibu wa kudumu wa mambo ya nje wa Kenya Dkt. Korir SingOei aliyesema kuwa mamlaka nchini Kenya haikufahamu au kushiriki katika kutiwa mbaroni na kisha kusafirishwa Uganda kwa Besigye.

Akizungumza Ijumaa, Novemba 22, waziri huyo Chris Baryomunsi alisema Serikali ya Uganda ilikuwa inawasiliana na serikali ya Kenya kabla ya kukamatwa kwa Besigye. Baryomunsi alisema kuwa haingewezekana kumkamata na kumsafirisha Besigye hadi Uganda kama mamlaka ya Kenya haikufahamu.

"Serikali ya Uganda ilikuwa inawasiliana na serikali ya Kenya, kama sivyo ungemkamataje mtu katikati ya Nairobi kisha kumrudisha Uganda kupitia uwanja wa ndege au hata kwa njia ya barabara bila ufahamu kamili na msaada wa serikali," alisema katika mahojiano na Televisheni ya NBS.

Besigye alikuwa nchini Kenya kwa ajili ya uzinduzi wa kitabu cha Martha Karua kabla ya kuwekwa chini ya ulinzi wa polisi kwa nguvu na kusafirishwa hadi jela ya kijeshi mjini Kampala. Kulingana na Martha Karua, mwanasiasa huyo alikuwa amefika Nairobi siku ya Jumamosi, Novemba 16, na kuingia katika Hoteli ya Waridi Paradise and Suites.

Besigye kisha aliondoka hotelini na dereva wa teksi kwa mkutano katika 108 Riverside Apartments na hapo ndipo alitoweka. Besigye alikuwa amepangiwa kuhudhuria na hata kuhutubia mkutano wa uzinduzi wa kitabu cha Martha Karua siku ya Jumapili Novemba 17, lakini alitiwa mbaroni kabla ya siku hiyo.


RADIO JAMBO FREQUENCIES

Kisumu 100.1 | Mombasa 92.3 | Nakuru 96.9 | Eldoret 99.5 | Nyeri 99.3 | Nyahururu 97.3 | Webuye 95.3 | Meru 92.7 | Kitui 104.9 | Kibwezi 104.7 | Voi 105.7 | Malindi 98.1 | Lamu 104.7 | Narok 97.3 | Kapenguria 99.7 | Kisii 89.3 | Garissa 104.3 | Maralal 97.3 | Lodwar 92.7


logo© Radio Jambo 2024. All rights reserved