logo

NOW ON AIR

Listen in Live

Charlene Ruto Awaomba Gen Z Kuwaheshimu Wazee

Charlene amekuwa akizungumza wazi kuhusu masuala muhimu yanayoikumba nchi, ikiwemo mauaji ya hivi karibuni ya Albert Ojwang.

image
na Tony Mballa

Habari21 June 2025 - 10:42

Muhtasari


  • Katika taarifa yake ya Ijumaa, Juni 20, 2025, binti huyo wa Rais alisema kuwa kizazi cha milenia kinaelewa vizazi vyote viwili, lakini kimeshindwa kuchukua hatua ya kuleta upatanisho.
  • Alisisitiza kuwa milenia wamekwepa jukumu lao la kuongoza na kuwaelekeza vijana, hali ambayo imechangia mivutano ya mara kwa mara nchini.

Binti wa Rais William Ruto, Charlene Ruto, amewashauri vijana wa kizazi cha Gen Z kujiepusha na mijadala isiyo na maana dhidi ya kizazi cha wazee.

Charlene aliwatuhumu vijana wa kizazi cha milenia kuwa ndio chanzo cha migogoro inayoendelea nchini kwa sasa, inayowakutanisha vijana wa Gen Z na wazee.

Katika taarifa yake ya Ijumaa, Juni 20, 2025, binti huyo wa Rais alisema kuwa kizazi cha milenia kinaelewa vizazi vyote viwili, lakini kimeshindwa kuchukua hatua ya kuleta upatanisho.

Charlene Ruto

Alisisitiza kuwa milenia wamekwepa jukumu lao la kuongoza na kuwaelekeza vijana, hali ambayo imechangia mivutano ya mara kwa mara nchini.

“Kwa sehemu, nawalaumu sisi milenia kwa migogoro ya mara kwa mara na isiyo na msingi kati ya wazee na vijana wa Gen Z. Sisi, kama kaka na dada wakubwa tunaowaelewa vizazi vyote, tumeshindwa kuingilia kati kuhakikisha maelewano ya pamoja, kutoa uongozi na mwelekeo nyakati za changamoto, na kuwaonyesha vijana wetu njia mbadala zisizohusisha ghasia, ambazo huishia tu kuongeza majeraha, kuchochea msimamo mkali na, kwa hali mbaya zaidi, kupoteza maisha,” ilisomeka sehemu ya taarifa ya Charlene Ruto.

Akiwahimiza milenia kuchukua jukumu lao ipasavyo, Charlene alisisitiza kuwa ni wakati wa taifa kukumbatia mazungumzo kama njia ya kushughulikia changamoto zinazoikumba nchi.

Binti huyo wa Rais alionya kuwa kuruhusu unyanyasaji wa mtandaoni kuna hatari ya kuvuruga mshikamano wa kijamii.

“Ni wakati tukumbatie usitishaji wa mivutano ya kizazi mara moja na tuanze kutumia njia mbadala zilizo na malengo ya kistaarabu kama mazungumzo ya kizazi tofauti, mapendekezo ya sera na kushinikiza mageuzi yenye busara,” Charlene alisisitiza.

“Ghasia, kulipiza kisasi, hasira zisizo na mwelekeo, utamaduni wa kufuta watu, fujo, unyanyasaji wa mtandaoni, na maandamano ya vurugu hayatatujenga bali yataharibu utamaduni wa taifa letu, kuchochea msimamo mkali miongoni mwa vijana, na kuleta hali hatarishi ya kutokuwa na utulivu.”

Charlene Ruto

Charlene amekuwa akizungumza wazi kuhusu masuala muhimu yanayoikumba nchi, ikiwemo mauaji ya hivi karibuni ya Albert Ojwang.

Jumamosi, Juni 14, 2025, Charlene alifichua kuwa aliwaomba vijana viongozi 106 waliokuwa kwenye kundi la wiki hii la mazungumzo kuhusu uongozi kusimama naye kwa dakika moja ya kimya kwa ajili ya kuenzi maisha ya Ojwang.

“Tunapohitimisha kundi la wiki hii la mazungumzo kuhusu uongozi, niliwaomba viongozi vijana 106 waliokuwepo wasimame nami kwa dakika moja ya kimya kwa ajili ya maisha ya Albert Ojwang. Kwa siku chache zilizopita nimekuwa nikitafakari kwa kina kuhusu kilichotokea,” Charlene alisema.

Charlene Ruto

Makala Zinazohusiana


RADIO JAMBO FREQUENCIES

Kisumu 100.1 | Mombasa 92.3 | Nakuru 96.9 | Eldoret 99.5 | Nyeri 99.3 | Nyahururu 97.3 | Webuye 95.3 | Meru 92.7 | Kitui 104.9 | Kibwezi 104.7 | Voi 105.7 | Malindi 98.1 | Lamu 104.7 | Narok 97.3 | Kapenguria 99.7 | Kisii 89.3 | Garissa 104.3 | Maralal 97.3 | Lodwar 92.7


logo© Radio Jambo 2024. All rights reserved