Familia ya marehemu Albert Ojwang’ imedai kuwa juhudi zao za kupata fedha kwa ajili ya maandalizi ya mazishi zilikutana na mshangao mkubwa baada ya kugundua kuwa kiasi kikubwa cha pesa kilikuwa kimetoweka kutoka kwa akaunti ya M-Pesa ya baba yake.
Familia hiyo ilisema kuwa fedha hizo, zilizochangwa kupitia mpango wa Sisi kwa Sisi ulioanzishwa na mchekeshaji Eric Omondi, ziliondolewa kutoka kwa akaunti ya M-Pesa ya baba yake bila idhini wala maelezo yoyote.
Tukio hilo la kusikitisha linafanana na tukio jingine lililomhusisha Boniface Kariuki, ambapo familia yake ilidai kupoteza KSh 200,000 kupitia udanganyifu unaohusiana na mpango huo wa Sisi kwa Sisi.
Kifo cha Ojwang’ akiwa mikononi mwa polisi kilizua ghadhabu ya kitaifa, huku Wakenya wengi wakitaka majibu kuhusu mazingira ya kifo chake chenye utata.
Wakati hisia zilipokuwa juu, maelfu ya Wakenya walijitokeza kuunga mkono familia hiyo iliyokuwa ikihuzunika, wakichangia kwa wingi kupitia mpango wa Sisi kwa Sisi unaoendeshwa na Eric Omondi.
Hata hivyo, katika mwelekeo wa kusikitisha, familia sasa inadai kuwa fedha hizo zilitoweka ghafla kutoka kwa akaunti ya M-Pesa ya baba wa marehemu, Meshack Opiyo.
Katika video iliyoshirikiwa na mtayarishaji wa YouTube Clinton Chirangah Shim, mjomba wa Ojwang’, Polycarp Odhiambo, alieleza kuhusu hali ngumu waliyoingia ambayo imeongeza uzito wa huzuni waliyo nayo.
“Siku chache zilizopita, kaka yangu alikwenda kutoa fedha lakini alipata matatizo kwa sababu hakuwa na kitambulisho. Alipoenda Safaricom kutafuta msaada, aligundua kuwa hata ile KSh 17,000 yake ya binafsi haikuwa tena. Walipochunguza taarifa ya miamala, waliona majina ya waliotoa pesa hizo. Zaidi ya KSh 500,000 zilikuwa zimepotea pamoja na kiasi chake mwenyewe,” Odhiambo alidai.
Aliongeza kuwa pesa zilizopotea zilikuwa zimekusanywa mahsusi kupitia jukwaa la Sisi kwa Sisi la Eric Omondi. Katika video hiyo hiyo, baba wa Albert, Meschak Ojwang’, anaonekana akiwa ameketi kwenye kiti, akionekana mwenye huzuni mkubwa na machozi, akitafakari kuhusu hasara hiyo.
Kisa hicho kinaakisi tukio lingine linalomhusu Boniface Kariuki, mchuuzi aliyeuawa kwa kupigwa risasi wakati wa maandamano ya hivi majuzi, na pia alikuwa mnufaika wa kampeni ya kuchangisha fedha iliyoendeshwa na Omondi.
Baba yake Kariuki hapo awali alidai kuwa alidanganywa na walaghai waliomtapeli zaidi ya KSh 200,000 kwa madai ya kumsaidia kujisajili katika mpango mpya wa Mamlaka ya Bima ya Afya ya Jamii (Social Health Authority).