
Gavana wa Homa Bay Gladys Wanga amewashambulia vikali viongozi wa upinzani ambao anadai wamekuwa wakimshambulia Waziri Mkuu wa zamani Raila Odinga ili wabaki na uhusiano wa kisiasa.
Wanga alisema kuwa wanasiasa hao wamekuwa wakimhusisha Raila katika kila mazungumzo ya kisiasa, hasa kufuatia maandamano ya hivi karibuni, badala ya kuwasilisha ajenda zao wenyewe.
“Hatuwezi kuwa na upinzani wa watu wa kula mizoga, watu wasiojua wanachokisema. Kazi yao ni kuzungumza tu kuhusu Baba. Kama hamna ajenda, shauri yenu,” alisema kwa ukali.
Aliyasema hayo wakati wa mazishi ya marehemu Albert Ojwang katika Shule ya Msingi ya Nyawango, Kaunti ya Homa Bay.
Katika kile kilichoonekana kama dongo kwa Naibu Rais wa zamani Rigathi Gachagua, gavana huyo alikumbusha jinsi Gachagua aliwahi kuapa kuweka mitego kumzuia Raila kujiunga na serikali.
Alisema kuwa serikali shirikishi ndiyo pekee inayoweza kuunganisha taifa.
Aidha, alidai kuwa baadhi ya viongozi wa kisiasa wamekuwa wakizunguka nchini bila mwelekeo, wakijaribu kunufaika kisiasa kutokana na nguvu ya harakati za kizazi cha Gen Z.
“Hawa Gen Z walitembea kwa uaminifu kwa ajili ya sababu ya kweli, inayohusu mustakabali wa taifa hili. Lakini hawatakubali mporwe sababu yao kwa ajili ya maslahi yenu binafsi,” aliongeza.
Kauli yake inajiri wakati viongozi wa upinzani wanaendelea na ziara katika eneo la Magharibi mwa Kenya
Viongozi hao wanatafuta uungwaji mkono chini ya kile wanachokitaja kama harakati ya “ukombozi wa kitaifa.”
Kiongozi wa chama cha Wiper Kalonzo Musyoka, Eugene Wamalwa wa DAP-K, na Mwanasheria Mkuu wa zamani Justin Muturi wanaongoza kampeni hiyo.
Alhamisi, waliandaa mikutano ya hadhara katika maeneo ya Kakamega na Vihiga.
“Kundi la wahuni lilitumwa kutuzuia, lakini walikutana na kizazi cha Gen Z kilichojaa ujasiri na uzalendo, waliosimama kidete bila kutetereka,” Kalonzo alisema.
Gachagua, kupitia chapisho katika mitandao ya kijamii, pia aliwashukuru wakazi wa Kakamega na Vihiga kwa kujitokeza kwa wingi.