

Mbunge wa Lang’ata, Felix Odiwuor almaarufu Jalang’o, ametangaza rasmi nia yake ya kugombea kiti cha Useneta wa Nairobi katika uchaguzi mkuu wa 2027.
Hatua inatarajiwa kumkutanisha ana kwa ana na Seneta wa sasa wa Nairobi na Katibu Mkuu wa Chama cha Orange Democratic Movement (ODM), Edwin Sifuna.
Akizungumza katika mahojiano na kituo kimoja cha redio cha humu nchini Jumanne, Februari 10, 2026, Jalang’o alieleza kwa mara ya kwanza hadharani azma yake ya kuwania wadhifa huo, akipuuza madai kuwa amesukumwa au kufadhiliwa kisiasa na Rais William Ruto.
Jalang’o Ajitetea Dhidi ya Madai ya Kupanikiwa Njia
Ingawa alichaguliwa kwa tiketi ya ODM, Jalang’o amekuwa akionekana mara kwa mara kuunga mkono ajenda za serikali ya Rais Ruto, hata kabla ya mazungumzo ya ushirikiano kati ya ODM na chama tawala cha UDA kuanza rasmi.
“Siasa haupangiwi na mtu yeyote. Kiti ambacho unakitaka haungoji kupangiwa au kuambiwa kwa sababu wewe ni rafiki wa mtu fulani. Ni uamuzi wako binafsi,” alisema Jalang’o.
Kauli hiyo imezua mjadala mkubwa ndani ya ODM, hasa miongoni mwa wanachama wanaoona msimamo wake kama kinyume na misingi ya jadi ya chama hicho kama upinzani.
Msimamo Wake Ndani ya ODM
Licha ya ukaribu wake unaoonekana na serikali ya sasa, Jalang’o alisisitiza kuwa bado ni mwanachama mwaminifu wa ODM na kwamba atagombea kwa tiketi ya chama hicho.
“Mimi ni mwana ODM, hicho ndicho chama changu na hapo ndipo niko. Ile coalition ambayo ODM itakuwa, hapo ndipo nitakuwa,” aliongeza.
Kauli hiyo inalenga kuwahakikishia wafuasi wa chama kuwa azma yake ya kisiasa haitoki nje ya mwavuli wa ODM, licha ya mazingira ya kisiasa yanayobadilika kwa kasi.
Mgawanyiko Ndani ya ODM Wajitokeza Wazi
Azma ya Jalang’o ya kumkabili Katibu Mkuu wa chama chake katika kinyang’anyiro cha Useneta inajiri wakati ambapo ODM inakabiliwa na mvutano wa ndani kuhusu uwezekano wa kushirikiana na chama tawala cha UDA.
Seneta Sifuna anaongoza mrengo unaopinga vikali ushirikiano huo, akionya kuwa unaweza kudhoofisha taswira na misingi ya ODM kama chama cha upinzani.
Kwa upande mwingine, Jalang’o anaonekana kuunga mkono mrengo unaohusishwa na Oburu Odinga, ambao unatetea kushirikiana na serikali kama njia ya kukuza maendeleo na utulivu wa kisiasa.
Kinyang’anyiro Kinachoashiria Mustakabali wa ODM
Iwapo kinyang’anyiro hicho kitaafikia hatua ya kura za mchujo ndani ya chama, basi ushindani kati ya Jalang’o—mtangazaji wa zamani wa redio na mbunge wa muhula wa kwanza—na Sifuna, wakili mashuhuri na mmoja wa viongozi wakuu wa kitaifa wa ODM, utaakisi zaidi ya siasa za Nairobi pekee.
Kwa wachambuzi wa siasa, pambano hilo linaonekana kama kura ya maoni juu ya mwelekeo wa baadaye wa ODM: kama itaendelea kujitambulisha kama chama cha upinzani mkali au itakubali nafasi mpya ndani ya muundo wa serikali.
Uchaguzi wa 2027, kwa mtazamo huo, unaweza kuamua si tu hatima ya kiti cha Useneta wa Nairobi, bali pia mwelekeo wa siasa za ODM kwa miaka ijayo.


