Miili 19 ya wahanga wa ajali ya ndege Tanzania yaagwa

Waziri mkuu Kassim Majaliwa aliongoza ibada hiyo na kutoa ahadi ya serikali kusimamia misiba ya wote hao.

Muhtasari

• Ndege ya Precision Air ilikuwa ikitoka jijini Dar es Salaam kuelekea Bukoba wakati hali mbaya ya anga iliiyumbisha na kuipelekea kuanguka katika ziwa Victoria.

Ibada ya walioangamia katika ajali ya ndege Bukoba
Ibada ya walioangamia katika ajali ya ndege Bukoba
Image: Mwananchi YouTube screengrab

Jumatatu mchana Kaitaba nchini Tanzania kuligubikwa na vilio, majonzi na simanzi katika ibada ya kuaga miili 19 ya wasafiri walioangamia katika ajali ya ndege ya Precision Air Jumapili katika ziwa Victoria.

Ibada ya wafu iliandaliwa katika uwanja wa Kaitaba ambapo viongozi mbali mbali walihudhuria huku hali ikiwa tete kwa majonzi na vilio.

Muongoni mwa waliohudhuria ibada hiyo ya msiba ni pamoja na waziri mkuu wa Tanzania Kassim Majaliwa ambaye alitoa ahadi kuwa serikali ya Jamhuri ya muungano wa Tanzania itasimamia gharama zote za mazishi ya wote walioangamia kwenye mkasa huo.

Ndege ya Precision Air ilikuwa ikitoka jijini Dar es Salaam kuelekea Bukoba wakati hali mbaya ya anga iliiyumbisha na kuipelekea kuanguka katika ziwa Victoria Jumapili asubuhi.

Abiria zaidi ya 40 walikuwa kwenye nndege hiyo ila 19 waliangamia ambao ibada ya kuaga miili yao ilifanyika Jumatatu.

Wasimamizi wa shirika hilo la ndege za kibiashara walisema kwamba hii ndio ilikuwa ajali mbaya zaidi kuwahi kutokea kwa ndege za Precision Air na kusema wanaziombea familia zote zilizoathirika na mkasa huo.

Waziri mkuu Majaliwa pia alimtambua kijana mmoja shujaa aliyefika wa kwanza na mashua yake na kufanya shughuli ya uokozi.

Kijana huyo aliyetambulika kwa jina Jackson Majaliwa alifanikiwa kuwaokoa watu wapatao 24 na waziri mkuu alimsema rais Suluhu alitoa agizo bwana huyo mdogo kupewa kazi katika jeshi la uoaoaji na zimamoto kama njia moja ya kuutambua mchango wake.