logo

NOW ON AIR

Listen in Live

Zimbabwe yashutumiwa kwa kuwaachilia 'wabakaji hatari' kwa msamaha

Rais Mnangagwa aliwasamehe wafungwa katika magereza 47 ya nchi hiyo katika jaribio la kupunguza msongamano.

image
na Radio Jambo

Yanayojiri25 May 2023 - 11:54

Muhtasari


•Imedaiwa wafungwa 4,000 walioachiwa huru kwa msamaha wa rais Mnangagwa wiki iliyopita wanajumuisha wabakaji watoto.

•Baadhi ya Wazimbabwe kwenye mitandao ya kijamii pia wametaka uamuzi huo kubatilishwa kwani unawaweka wanawake katika hatari.

Muungano wa upinzani nchini Zimbabwe Citizens Coalition for Change (CCC) umedai kuwa zaidi ya wafungwa 4,000 walioachiwa huru kwa msamaha wa rais wiki iliyopita wanajumuisha wabakaji watoto.

Rais Emmerson Mnangagwa aliwasamehe wafungwa waliotoka katika magereza 47 ya nchi hiyo katika jaribio la kupunguza msongamano.

Mamlaka za magereza hata hivyo zilisema, ubakaji ni miongoni mwa makosa ambayo hayakujumuishwa katika msamaha huo.

Video zilizosambazwa mtandaoni zilionyesha kile ambacho vyombo vya habari vya nchini humo vilisema ni wabakaji wakisherehekea uhuru wao huku baadhi yao wakisemekana kuwa wametumikia hukumu yao kwa chini ya mwaka mmoja.

CCC katika taarifa yake siku ya Jumatano ilisema "haikuwa sawa kuwaachilia wahalifu hatari na ambao hawajarekebishwa kujumuika tena na jamii" kabla ya kuwaarifu au kuwatayarisha kisaikolojia waathiriwa wa ubakaji.

"Kumwachilia mbakaji ambaye hajarekebisha maadili yake katika jamii bila ulinzi wowote wa kuwalinda waathiriwa kunahatarisha wanawake na wasichana na kamwe hakuwezi kuwa na sababu za msingi katika jamii ya kidemokrasia," msemaji wa CCC Fadzayi Mahere alisema.

Baadhi ya Wazimbabwe kwenye mitandao ya kijamii pia wametaka uamuzi huo kubatilishwa kwani unawaweka wanawake katika hatari.

Mwanahabari mashuhuri wa uchunguzi Hopewell Chin’ono alisema msamaha "kamwe hautolewi kwa wabakaji au watu ambao wamefanya uhalifu wa kikatili".

Bw Chin’ono, mkosoaji wa serikali, alisema wanawake wa Zimbabwe hawatakuwa salama kufuatia msamaha huo.

Mamlaka za Zimbabwe bado hazijatoa maoni yoyote kuhusu madai hayo.


RADIO JAMBO FREQUENCIES

Kisumu 100.1 | Mombasa 92.3 | Nakuru 96.9 | Eldoret 99.5 | Nyeri 99.3 | Nyahururu 97.3 | Webuye 95.3 | Meru 92.7 | Kitui 104.9 | Kibwezi 104.7 | Voi 105.7 | Malindi 98.1 | Lamu 104.7 | Narok 97.3 | Kapenguria 99.7 | Kisii 89.3 | Garissa 104.3 | Maralal 97.3 | Lodwar 92.7


logo© Radio Jambo 2024. All rights reserved