logo

NOW ON AIR

Listen in Live

Kwa nini Rais aliyesimamishwa kazi wa Korea Kusini hakamatiki?

Amri ya hali ya hatari ya Yoon ilifuatiwa na kura ya kusimamishwa kazi ikafuata.

image
na BBC NEWS

Kimataifa04 January 2025 - 15:08

Muhtasari


  • Kiongozi huyo wa mrengo wa kulia bado ana wafuasi wengi wanao muunga mkono - na maelfu walijitokeza nje ya nyumba yake Ijumaa asubuhi kupinga kukamatwa kwake.


Kulikuwa na zaidi ya maafisa 100 wa polisi wa Korea Kusini na walikuwa na kibali cha kumkamata - lakini wameshindwa kumkamata Rais aliyesimamishwa kazi Yoon Suk Yeol baada ya vute nikuvute ya saa sita nje ya nyumba yake.

Ndio muda ambao makabiliano kati ya timu ya usalama ya Yoon na maafisa hao yalivyodumu, walitengeneza ukuta wa watu na kutumia magari kuziba njia, kulingana na vyombo vya habari vya ndani.

Amri ya hali ya hatari ya Yoon ilifuatiwa na kura ya kusimamishwa kazi ikafuata. Kisha ukaja uchunguzi wa makosa ya jinai, kukataa kwake kuhojiwa, na sasa amekataa hata kukamatwa, huku akisubiri uamuzi wa mahakama ya kikatiba ambao unaweza kumuondoa madarakani.

Kiongozi huyo wa mrengo wa kulia bado ana wafuasi wengi wanao muunga mkono - na maelfu walijitokeza nje ya nyumba yake Ijumaa asubuhi kupinga kukamatwa kwake.

Walinzi wake

tr

Chanzo cha picha,Reuters

Maelezo ya picha,Waandamanaji wakabiliana na polisi baada ya maafisa kushindwa kumkamata rais aliyesimamishwa kazi

Ingawa Yoon amepokonywa mamlaka yake ya urais - baada ya wabunge kupiga kura ya kumuondoa - lakini bado ana haki ya kupata usalama. Na watu wake wa usalama walichangia pakubwa katika kuzuia kukamatwa siku ya Ijumaa.

Mason Richey, profesa katika Chuo Kikuu cha Hankuk cha Seoul anasema, "ingawa timu ya ulinzi wa rais (PSS) inapaswa kuchukua maelekezo kutoka kwa kaimu Rais Choi Sang-mok. Huenda hawajaagizwa na kaimu Rais Choi kuruhusu akamatwe, au wanakataa maagizo yake."

Baadhi ya wataalam wanaamini walinzi wake huenda wanaonyesha "uaminifu" kwa Yoon, kwa kuwa mkuu wa PSS, Park Jong-joon aliteuliwa kwa kazi hiyo na Yoon Septemba iliyopita.

"Inawezekana Yoon ameweka watu watiifu sana katika timu hiyo katika kujiandaa na tukio hili," anasema mwanasheria mwenye makao yake Marekani na mtaalamu masuala ya Korea, Christopher Jumin Lee.

Na mtangulizi wa Park alikuwa waziri wa zamani wa ulinzi Kim Yong-hyun, ambaye anashutumiwa kwa kumshauri Yoon kutangaza hali ya hatari. Kwa sasa anashikiliwa kwa mahojiano kama sehemu ya uchunguzi wa uhalifu wa Yoon.

Hatari ya mvutano kuongezeka

trgv

Chanzo cha picha,Getty Images

Maelezo ya picha,Maafisa wa polisi wawaondoa wafuasi wa Rais wa Korea Kusini aliyeondolewa madarakani Yoon Suk Yeol nje ya makazi yake rasmi mjini Seoul.

Suluhu "rahisi", Lee anasema, ni kwa kaimu rais Choi kuamuru PSS iruhusu akamatwe. "Ikiwa hataki kufanya hivyo, hiyo inaweza kuwa sababu na yeye kushtakiwa na Bunge," aliongeza.

Choi, ambaye ni waziri wa fedha, ameshika nafasi hiyo baada ya wabunge kupiga kura ya kumwondoa mrithi wa kwanza wa Yoon, Waziri Mkuu Han Duck-soo.

Mkwamo huu wa kisiasa unaonyesha mgawanyiko katika siasa za Korea Kusini - kati ya wale wanaomuunga mkono Yoon, na uamuzi wake wa kuweka sheria ya hali ya hatari, na wale wanaoipinga.

Idadi kubwa ya Wakorea Kusini wanakubali kwamba tamko la Yoon la sheria ya hali ya hatari Desemba 3 lilikuwa la makosa na anahitaji kuwajibika, anasema Duyeon Kim, mtaalamu wa masuala ya usalama.

PSS pia ina silaha nzito, kwa hivyo maafisa wanaotaka kumkamata rais hawataki mzozo uongezeke.

"Ni nini kitatokea ikiwa polisi watajitokeza na vibali vya ziada vya kutaka kukamatwa kwa maafisa wa PSS, na [PSS] wakakaidi vibali hivyo na kisha kufyatua bunduki zao?" anauliza Lee.

Wakati marais wa Korea Kusini wamefungwa hapo awali, Yoon ndiye wa kwanza kukamatwa kabla ya kujiuzulu. Maafisa wana hadi Januari 6 kumkamata Yoon kabla ya hati ya sasa kuisha.

Wanaweza kujaribu kumkamata Yoon tena mwishoni mwa juma, ingawa wikendi inaweza kuleta changamoto kubwa ikiwa umati wa wafuasi utaongezeka. Wanaweza pia kutuma maombi ya hati mpya na kujaribu kumkamata tena.


RADIO JAMBO FREQUENCIES

Kisumu 100.1 | Mombasa 92.3 | Nakuru 96.9 | Eldoret 99.5 | Nyeri 99.3 | Nyahururu 97.3 | Webuye 95.3 | Meru 92.7 | Kitui 104.9 | Kibwezi 104.7 | Voi 105.7 | Malindi 98.1 | Lamu 104.7 | Narok 97.3 | Kapenguria 99.7 | Kisii 89.3 | Garissa 104.3 | Maralal 97.3 | Lodwar 92.7


logo© Radio Jambo 2024. All rights reserved