
Rais wa Marekani, Donald Trump ametia saini amri ya kulifunga shirika la habari linalofadhiliwa na serikali ya Sauti ya Amerika, akikishutumu kuwa "kumpinga Trump" na "lenye msimamo mkali".
Taarifa ya Ikulu ya White House ilisema amri hiyo "itahakikisha walipakodi hawako tena kwenye ndoano ya propaganda kali", na kujumuisha nukuu kutoka kwa wanasiasa na vyombo vya habari vya mrengo wa kulia vinavyokashifu VOA ya "mrengo wa kushoto",
VOA, ambayo bado ni huduma ya redio, ilianzishwa wakati wa Vita vya Pili vya Dunia ili kukabiliana na propaganda za Nazi.
Inatumiwa na mamia ya mamilioni ya watu duniani kote. Mike Abramowitz, mkurugenzi wa VOA, alisema yeye na takribani wafanyakazi wake wote, watu 1,300 walikuwa wamepewa likizo ya malipo.
Abramowitz alisema kuwa amri hiyo iliifanya VOA kushindwa kutekeleza "dhamira yake muhimu... muhimu sana...hasa muhimu leo, wakati wapinzani wa Marekani, kama Iran,China, na Urusi, wanazamisha mabilioni ya dola katika kuunda simulizi za uwongo ili kuidharau Marekani".
Amri ya rais inalenga kampuni mama ya VOA ya US Agency for Global Media, au USAGM, ambayo pia inafadhili mashirika yasiyo ya faida kama vile Radio Free Europe na Radio Free Asia, ambayo awali yalianzishwa ili kukabiliana na ukomunisti.
Inawaambia wasimamizi "kupunguza utendakazi… kwa kiwango cha chini kabisa cha uwepo na utendakazi unaohitajika kisheria". CBS, mshirika wa habari wa BBC nchini Marekani, ilisema kuwa wafanyakazi wa VOA waliarifiwa katika barua pepe na Crystal Thomas, mkurugenzi wa rasilimali watu wa USAGM.
Chanzo kimoja kilisema kwamba wafanyakazi wote wa kujitegemea na wa kimataifa waliambiwa sasa hakuna pesa za kuwalipa.
Barua pepe zilizotazamwa na CBS ziliarifu wakuu wa Radio Free Asia na Radio Free Europe/Radio Liberty kwamba ruzuku zao za serikali zimekatishwa.
VOA na vituo vingine vilivyo chini ya USAGM vinahudumia zaidi ya wasikilizaji 400,000,000 na kwa upana ni sawa na BBC World Service, ambayo inafadhiliwa kwa sehemu na serikali ya Uingereza.
Elon Musk, bilionea na mshauri mkuu wa Trump ambaye amekuwa akisimamia upunguzaji mkubwa wa wafanyakazi wa serikali ya Marekani, ametumia mtandao wake wa kijamii wa X kutaka VOA ifungwe.